Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akielezea kuhusu Hali ya Uchumi wa Taifa na utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2018/2019 katika kipindi cha Julai-Novemba, 2018), ambapo alisema Tanzania inaendelea kuwa miongoni mwa nchi tano zinazokua kwa kasi kiuchumi Barani Afrika, wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma.

WAZIRI MPANGO ATOA TAARIFA HALI YA UCHUMI NA UTEKELEZAJI WA BAJETI KUU YA SERIKALI 2018/2019

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO

Ad

HALI YA UCHUMI WA TAIFA NA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI

30 Desemba 2018, Dar es salaam.

  1. Pato la Taifa (kwa bei za 2007)
  • Uchumi wa Taifa umeendelea kuwa imara, ukikua kwa 7.1% (2017) ikilinganishwa na wastani wa ukuaji wa 7.0% kwa miaka miwili iliyopita (2015-2016).
  • Kwa nchi za EAC, uchumi wa Tanzania ulikua kwa kasi zaidi (7.1%) mwaka 2017 ukilinganisha na Rwanda (6.1%), Uganda (5.1%), Kenya (4.9%), na Burundi (0.0%). Vilevile, Tanzania iliongoza katika ukuaji wa uchumi kwenye nchi za SADC.
  • Katika kipindi cha Januari hadi Juni 2018, Pato la Taifa lilikua kwa 7.0% ikilinganishwa na 6.3% katika kipindi kama hicho mwaka 2017. Sekta zilizokua kwa kasi zaidi ni: ujenzi (15.7%), Uzalishaji viwandani (12.0%), habari na mawasiliano (11.2), na uchukuzi & uhifadhi mizigo (8.2%).
  • Aidha, Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa nchi 5 bora kwa kasi ya ukuaji wa uchumi katika bara la Afrika katika nusu ya kwanza ya 2018, ikijumuisha: Ethiopia (8.5%), Ivory Coast (7.4%), Rwanda (7.2), Tanzania (7.0%), na Senegal (7.0%).
  • Sekta zilizoendelea kutoa mchango mkubwa katika Pato la Taifa (Januari – Juni 2018) ni Kilimo (34.5%), Ujenzi (16.8%) na Biashara (10.1%). Aidha, sekta ya kilimo ilikua kwa 3.6% kwa kipindi hicho. Napenda kwa niaba ya Serikali kuwapongeza wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya ujenzi kwa mchango wao mkubwa katika uchumi wa Taifa.
  1. Mfumuko wa Bei
  • Mfumuko wa bei umeendelea kupungua kutoka wastani wa 4.3% mwaka 2017/18 hadi kufikia kiwango cha chini kabisa kuwahi kutokea katika miaka ya karibuni cha 3.0% mwezi Novemba 2018. Lengo la kipindi cha muda wa kati ni 5%.
  • Kati ya Julai hadi Novemba 2018, Tanzania ilikuwa na kiwango kidogo zaidi cha mfumuko wa bei ikilinganishwa na Uganda (3.3%) na Kenya (4.8%).
  • Sababu zilizochangia mfumuko wa bei kuwa chini ni pamoja na:
    • Upatikanaji mzuri wa chakula katika masoko ya ndani na nchi jirani, ambapo uzalishaji wa chakula nchini ulifikia tani 15.9m ikilinganishwa na mahitaji ya tani 13.3m kwa kipindi hicho, hivyo kuwa na utoshelevu wa chakula kwa 120%. Mfumuko wa bei ya chakula ulifikia 2.0% Novemba 2018 ikilinganishwa na 7.9% katika kipindi kama hicho mwaka 2017;
    • Kutengamaa kwa bei za mafuta katika soko la dunia; na
    • Utekelezaji madhubuti wa sera za fedha na za bajeti.
  1. Hali ya maisha ya mwananchi
  • Kasi kubwa ya ukuaji wa uchumi imepelekea kuimarika kwa hali ya maisha ya wananchi hasa wale waliopata fursa za ajira (na kipato) katika shughuli za kiuchumi zinazokua haraka, kama vile ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara, reli, upanuzi wa bandari na viwanja vya ndege, mauzo ya mazao ya kilimo, ujenzi wa viwanda na utoaji wa huduma za fedha na mawasiliano. Kuongezeka kwa ujenzi wa nyumba bora za kuishi, umiliki wa mali zisizohamishika na vyombo vya usafiri, na vifaa vya kudumu vya majumbani (consumer durables) vinaashiria kuimarika kwa hali ya maisha ya wananchi.
  • Aidha, ukuaji mzuri wa uchumi umeiwezesha Serikali kuongeza ukusanyaji wa mapato na kugharamia uboreshaji wa huduma za jamii hususan elimu (ikwemo elimu-msingi bila ada), afya (hospitali, vituo vya afya, zahanati, madawa, vifaa-tiba, vitendanishi), maji na kuimarisha uzalishaji wa umeme na kuusambaza vijijini.
  • Kutokana na kiwango kidogo cha mfumuko wa bei, uwezo wa shilingi kununua vitu ni mkubwa (Nguvu ya buku 10 acha kabisa!). Aidha, gharama za maisha kwa mwananchi kwa ujumla, zimeongezeka kwa kasi ndogo.
  1. Thamani ya Shilingi
  • Thamani ya shilingi ya Tanzania imeendelea kuwa tulivu. Katika kipindi cha kuanzia mwezi Julai hadi Novemba 2018, dola moja ya Marekani ilibadilishwa kwa wastani wa shilingi 2,276, ikilinganishwa na shilingi 2,235 katika kipindi cha Julai hadi Novemba 2017. Hivyo, shilingi ilipungua thamani dhidi ya dola (depreciation) kwa asilimia 1.8, kiwango ambacho ni kidogo na hakikuathiri utulivu wa thamani ya shilingi ya Tanzania ikizingatiwa kuwa mfumuko wa bei wa wastani katika nchi washirika wakuu wa biashara na Tanzania ni asilimia 3.0.
  • Utulivu wa thamani ya shilingi umetokana na utekelezaji wa sera ya fedha, usimamizi thabiti wa mapato na matumizi ya Serikali, kutumia gesi asilia katika kuzalisha umeme, na baadhi ya viwanda kuzalisha bidhaa ambazo awali zilikuwa zikiagizwa kwa wingi kutoka nje, mfano,
  1. Utekelezaji wa Sera ya Fedha
  • Katika kipindi cha nusu ya kwanza ya mwaka 2018/19, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania ilichukua hatua mbalimbali kuongeza ukwasi kwenye uchumi ili kuziwezesha benki za biashara kuongeza utoaji wa mikopo kwa sekta binafsi. Miongoni mwa hatua hizo ni:
    • Kutoa mikopo ya muda mfupi kwa mabenki;
    • Kushusha riba ya mikopo kwa mabenki kutoka 9.0% hadi 7.0% Agosti 2018; na
    • Kununua fedha za kigeni kutoka katika benki za biashara & taasisi za Serikali;
  • Kutokana na hatua hizo, ukwasi kwenye mabenki ya biashara uliongezeka na riba katika masoko ya fedha zilipungua.
    • Riba ya siku moja katika soko la fedha baina ya mabenki ilishuka kutoka 3.72% Oktoba 2017 hadi wastani wa 2.29% Oktoba 2018.
    • Riba za dhamana za Serikali zilipungua kutoka 9.41% hadi kufikia wastani wa 7.40% Oktoba 2017.
    • Riba za mikopo inayotolewa na mabenki ilipungua kwa kiasi kidogo kutoka wastani wa 18.1% kati ya Julai na Oktoba 2017 hadi 17.3% katika kipindi kama hicho mwaka 2018.
  • Ukuaji wa ujazi wa fedha (M3) uliimarika na kuwa wastani wa 6.1% (Julai – Oktoba 2018) ukilinganisha na 5.0% katika kipindi kama hicho 2017. Ukuaji huu uliendana na mahitaji ya uchumi.
  • Ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi uliongezeka kwa wastani wa 4.6% (Julai hadi Oktoba 2018) ukilinganisha na wastani wa 0.2% kwa kipindi kama hicho mwaka 2017.
  1. Akiba ya Fedha za Kigeni
  • Akiba ya fedha za kigeni imeendelea kuwa ya kuridhisha na kutosheleza mahitaji ya kuiwezesha Tanzania kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje na pia kujenga imani ya wawekezaji.
  • Akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Marekani milioni 5,079.0 mwezi Novemba 2018, kiasi ambacho kinatosha kugharamia uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa kipindi cha takriban miezi 5.
  • Kiwango hiki cha akiba ya fedha za kigeni ni zaidi ya lengo la Serikali kuwa na akiba ya fedha za kigeni inayokidhi uagizaji wa bidhaa na huduma kwa miezi 4. Pia ni zaidi ya lengo la miezi 4.5 lililowekwa kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
  1. Mwenendo wa Sekta ya Kib
  • Sekta ya kibenki imeendelea kuwa imara, salama na yenye kutengeneza faida, ikiwa na mitaji na ukwasi wa kutosha zaidi ya kiwango kinachotakiwa kisheria.
  • Uwiano wa mitaji ya mabenki ikilinganishwa na rasilimali zao ulikuwa 16.3%, ikiwa juu ya kiwango kinachohitajika kisheria cha 10.0%.
  • Kiwango cha mali inayoweza kubadilishwa kuwa fedha taslimu ikilinganishwa na kiwango cha amana zinazoweza kuhitajika katika muda mfupi kilifikia 36% ikilinganishwa na kiwango cha chini kinachohitajika kisheria cha 20%.

Hii inaashiria kuwa mabenki yana ukwasi wa kutosha kwa ajili ya shughuli zake za kila siku ikiwemo kulipa madeni pamoja na kutoa mikopo.

  • Katika kipindi cha Januari hadi Novemba 2018, sekta ya kibenki ilipata faida ya shilingi bilioni 285.4 (ikilinganishwa na shilingi bilioni 317.0 katika kipindi kama hicho mwaka 2017). Kupungua kwa faida kulitokana na kuongezeka kwa tengo la hasara kufuatia kuanza kutumika kwa Kanuni za Kimataifa za Utoaji Taarifa za Fedha (International Financial Reporting Standard 9 – IFRS9) mwezi Januari 2018.
  • Mikopo chechefu iliendelea kushuka hadi kufikia 9.7% ya mikopo yote Septemba 2018 kutoka 12.5% iliyorekodiwa mwishoni mwa Disemba 2017.
  • Kuendelea kupungua kwa mikopo chechefu kulitokana na hatua zilizochukuliwa na BoT   ikiwa pamoja na:
    • Kuzitaka benki zote kutekeleza mikakati ya kuboresha utoaji na usimamizi wa mikopo, ikiwemo uchambuzi wa maombi ya mikopo, na kutumia kwa lazima taarifa ya historia za wakopaji kabla ya kutoa mkopo; na
    • Benki zote kutakiwa kuazisha idara maalum kwa ajili ya kufuatilia ukusanyaji wa madeni chechefu.
  • Sekta ya kibenki pia imeendelea kukua. Hadi Septemba 2018, kulikuwa na jumla ya Benki na Taasisi za fedha zinazosimamiwa na BOT zipatazo 61. Kati ya hizo, mabenki yalikuwa 52 yenye matawi 884 nchini kote na zingine zilikuwa taasisi zinazotoa huduma za kifedha.
  1. Maduka ya Kubadilisha Fedha za Kigeni
  • Serikali kupitia BoT imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha biashara ya maduka ya kubadilisha fedha za kigeni ili kuondoa uwezekano wa maduka haya kufanya biashara isiyo halali ambayo ni pamoja na utakatishaji wa fedha haramu.
  • Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na BoT kufanya msako wa kukagua maduka haya Arusha na kubaini baadhi ya mambo ambayo yalikuwa yanafanywa na maduka haya kinyume na leseni zao. Zoezi hili litakuwa endelevu ili kuhakikisha kwamba mwenendo wa maduka haya unaridhisha.
  • Mwezi Juni 2017, BOT ilifanya mabadiliko ya Kanuni za Biashara ya Maduka ya Kubadilisha Fedha za Kigeni ya mwaka 2015 kwa lengo la kuboresha usimamizi na kudhibiti matumizi mabaya ya maduka haya. Hivyo, kiwango cha chini cha mtaji wa maduka yaliyoko katika Daraja A kiliongezwa kutoka Tshs. 100mn hadi Tshs. 300mn na Daraja B kutoka Tshs. 250m hadi Tshs. 1bn.
  • Kabla ya zoezi la usajili upya wa maduka hayo, kulikuwa na maduka 297 nchi nzima. Baada ya zoezi la usajili, maduka 109 tu ndio yalikidhi vigezo husika na kupewa leseni mpya. Jumla ya maduka 188 yalishindwa kutimiza masharti na hivyo kupelekea kufutiwa leseni.
  1. Mwenendo wa Sekta ya Biashara Nje (Julai – Nov 2018)
  • Thamani ya mauzo nje (traditional & non traditional exports) ilifikia USD 1,939.2mn (Julai – November 2018) ikilinganishwa na USD 2,194.4mn katika kipindi kama hicho mwaka 2017.
  • Thamani ya bidhaa zilizonunuliwa kutoka nje (Capital, intermediate & consumer goods f.o.b.) iliongezeka kutoka USD 3,310.1mn (Julai – Novemba 2017) hadi USD 3,483.4mn (Julai – Novemba 2018).
  • Nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa, huduma na uhamisho mali nchi za nje (current account deficit) iliongezeka na kufikia USD 701.0mn ikilinganishwa na nakisi ya USD 580.4mn katika kipindi kama hicho mwaka 2017/18.
  • Kuongezeka kwa nakisi kulitokana na:
    • Kuongezeka kwa thamani ya bidhaa za mitaji zilizoagizwa kutoka nje ya nchi (kutoka USD 1,097mn hadi USD 1,408.8mn) kwa ajili ya miradi mikubwa ya maendeleo, hasa ile ya ujenzi wa reli ya kisasa na barabara.
    • Kupungua kwa mapato yatokanayo na bidhaa zilizouzwa nje ya nchi kulikochangiwa na sababu mbalimbali, hasa ile ya kushuka kwa bei za mazao mengi katika soko la dunia.
  1. Mwenendo wa Utekelezaji wa Bajeti ya Serikali
  • Mapato ya Serikali
  • Katika kipindi cha miezi mitano ya kwanza ya mwaka 2018/19 (Julai – Novemba), makusanyo ya ndani (ikijumuisha mapato ya Halmashauri) yalifikia Ths. 7.37tn sawa na 88.9% ya makadirio ya Tshs. 8.30tn katika kipindi hicho.
  • Mapato ya kodi yalifikia Tshs. 6.23tn ikiwa ni 88% ya lengo la kukusanya Tshs.7.04tn kwa kipindi hicho.
  • Mapato yasiyo ya kodi yalifikia Ths. 936.03bn sawa na 21% zaidi ya lengo la Tshs.775.36bn
  • Mapato ya Halmashauri yalifikia Tshs.8bn sawa na 61% ya lengo.
  • Ongezeko la mapato yasiyo ya kodi limetokana na kuimarishwa kwa ufuatiliaji kwenye Taasisi, Mashirika na Kampuni kulikoiwezesha Serikali kupata michango na gawio stahiki kutoka kwenye uwekezaji wake; Kuimarika kwa matumizi ya Technolojia katika ukusanyaji wa maduhuli kwenye Wizara na Idara zinazojitegemea kupitia Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato uitwao Government Electronic Payment Gateway (GePG) ambapo kati ya Julai 2017 hadi Novemba 2018, jumla ya Taasisi za Serikali 325 zinatumia mfumo huu kukusanya maduhuli.
  • Jitihada za kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara: Serikali kupitia Sheria ya Fedha 2018/19 Serikali ilipunguza ada na tozo mbalimbali ambazo zilikuwa kero kwa wananchi. Miongoni mwa ada na tozo zilizopunguzwa ni pamoja na tozo za mazingira, OSHA, FIRE, TBS, TFDA na tozo kwenye madini ya chumvi.
  • Changamoto za ukusanyaji wa mapato ni pamoja na ukwepaji wa kodi; mwamko mdogo wa wananchi kudai risiti pale wanapofanya manunuzi na wafanyabiashara kutoa risiti pale wanapofanya mauzo; na wigo mdogo wa kodi.
  • Misaada na Mikopo Nafuu
  • Washirika wa Maendeleo wameendelea kusaidia bajeti ya Serikali kupitia miradi na programu mbalimbali. 2017/18, Washirika wa Maendeleo waliahidi kuchangia Bajeti ya Serikali kiasi cha Tshs. 3.97tn. Hadi kufikia Juni 2018, Washirika wa maendeleo walitoa Tshs. 2.46tn ambazo ni sawa na asilimia 62 ya ahadi.
  • Katika mwaka 2018/19, Washirika wa Maendeleo wameahidi kuchangia bajeti ya Serikali kiasi cha Tshs. 2.67tn. Hadi kufikia Novemba, 2018, kiasi cha Tshs. 498.5bn kimepokelewa, sawa na asilimia 54 ya kiasi cha Tshs 928.7bn kilichotarajiwa katika kipindi cha Julai hadi Novemba 2018.
  • Kasi ndogo ya utoaji fedha inatokana na:
    • Masharti magumu ya wafadhili na majadiliano kuchukua muda mrefu.
    • Kasi ndogo ya utekelezaji wa baadhi ya miradi katika sekta na hivyo kusababisha fedha za awamu zinazofuata kuchelewa kutolewa;
  • Matumizi ya Serikali
  • Bajeti iliyoidhinishwa na Bunge kwa mwaka 2018/19 ni Tshs. 32.47tn ikijumuisha Tshs. 20.46tn za matumizi ya kawaida na Tshs. 12.00tn matumizi ya maendeleo.
  • Kati ya Julai hadi Novemba, 2018, Serikali imetumia jumla ya Tshs.10.41tn, sawa na asilimia 79 ya lengo la Tshs. 13.22tn kwa kipindi hicho.
  • Kati ya kiasi hicho, Tshs. 8.29tn ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida (bila kujumuisha makusanyo ya Halmashauri) sawa na 99% ya lengo la Tshs. 8.36tn.
    • 2.86tn zilikuwa za mishahara, sawa na asilimia 93 ya lengo la Tshs. 3.08tn; na fedha za matumizi mengineyo (OC) zilikuwa Tshs. 5.42tn sawa na 103% ya lengo la Tshs. 5.27tn.
  • Fedha za maendeleo zilikuwa Tshs. 2.12tn
  • Katika Utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kipaumbele kilitolewa katika maeneo yafuatayo:
    • Utekelezaji wa miradi ya miundombinu ya barabara, reli na viwanja vya ndege (Tshs. 638.23bn);
    • Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya Juu, uimarishaji wa vyuo vya VETA na kukuza ujuzi kwa vijana Tshs. 226.76bn);
    • Utekelezaji wa miradi ya maji na umeme vijijini (Tshs. 185.68bn);
    • Miradi ya afya, ununuzi wa dawa, chanjo, viatilifu na vitendanishi na ujenzi/ukarabati wa hospitali (Tshs. 179.86bn);
    • Kukamilisha malipo ya ndege mpya mbili aina ya Airbus A220 – 300 ambapo moja imewasili nchini tarehe 24 Disemba (Tshs. 152.1bn); na
    • Kugharamia Elimu-msingi bila malipo (Tshs. 104.03bn).
  • Serikali iliendelea kulipa madai mbalimbali jumla ya Tshs 331.79bn kama ifuatavyo:
    • Wazabuni Tshs. 132.72bn; Wakandarasi Tshs. 175.37bn; na Watumishi Tshs. 23.7bn.
  1. Deni la Serikali
  • Kufikia Sept. 2018 deni la Serikali lilifikia Tshs. 49.37tn (sawa na ongezeko la 3.2%) ikilinganishwa na Tshs. 47.82tn Sept. 2017
  • Deni la ndani lilikuwa Tshs. 13.64tn (27.6%)
    • Deni la nje Tshs. 35.72tn (72.4%)
  • Mikopo hii imetumika kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo:
    • Ujenzi wa bomba la gesi Mtwara – Dar es Salaam;
    • Ujenzi na ukarabati wa miondombinu ya barabara, madaraja, reli na bandari;
    • Ujenzi wa mitambo ya kufua umeme (Ubungo, Mwanza na Kinyerezi II);
    • Miradi ya maji, (ikijumuisha mradi wa Maji ziwa Victoria);
    • Miradi ya TASAF;
    • Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano; na
    • Mradi wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere.
  • Nchi kuwa na deni sio dhambi, jambo muhimu ni kuhakikisha kuwa fedha tulizokopa zinatumika kujenga rasilimali ambazo ni msingi wa kuongeza uwezo wetu wa kuzalisha mali na kulipa mikopo hiyo.
  1. Uhimilivu wa Deni
  • Kwa mujibu wa Sheria ya Mikopo Dhamana na Misaada Sura 134, Serikali inawajibu wa kufanya tathmini ya uhimilivu wa deni (DSA) kila mwaka ili kupima mwenendo wa deni na uhimilivu wake.
  • Matokeo ya awali ya tathmini iliyofanywa Desemba 2018 inaonesha kuwa deni ni himilivu kwa muda mfupi, wa kati na mrefu. Matokeo haya yanafanana na tathmini iliyofanywa na IMF. Deni la umma limeendelea kuwa himilivu.
  • Katika tathmini hiyo, viashiria vinaonesha uwiano ufuatao kwa thamani ya sasa (Present Value Terms):
    • Deni la Serikali kwa GDP 27.2% ikilinganishwa na ukomo wa 70%;
    • Uwiano wa deni la nje kwa GDP (22.2%) ikilinganishwa na ukomo wa 55%;
    • Deni la nje kwa mauzo nje 157.3% ikilinganishwaa na ukomo wa 240%;
    • Ulipaji wa deni la nje kwa kutumia mauzo ya bidhaa nje 15.2% ikilinganishwa na ukomo wa 23%; na
    • Ulipaji wa deni kwa mapato ya ndani 49.6%.
  • Viashiria vyote vinaonesha kuwa Serikali ina uwezo wa kuendelea kukopa na kulipa pale mikopo inapoiva.
  • Serikali itaendelea kusimamia deni na kuhakikisha kuwa linaendelea kuwa himilivu:
  • Mikopo itaelekezwa kugharamia miradi ya maendeleo yenye tija kwa Taifa na ambayo inachochea ukuaji wa uchumi;
    • Kuweka kipaumbele kukopa mikopo yenye masharti nafuu na kuhakikisha mikopo ya masharti ya kibiashara inakopwa kwa uangalifu mkubwa na kwamba inatumika kwenye maeneo ambayo yanachochea ukuaji wa uchumi;
    • Kuboresha ukusanyaji wa mapato (ya kodi na yasiyo ya kodi), hususan kwa kuziba mianya ya uvujaji wa mapato na kupanua wigo ili kuhakikisha sehemu kubwa ya bajeti inagharamiwa na mapato ya ndani pamoja na kupunguza matumizi yanayoweza kuepukika; na
    • Kusimamisha utoaji wa Dhamana za Serikali kwa Taasisi za Serikali ambazo zinategemea ruzuku kujiendesha.
  1. Matarajio Hadi Juni 2019

Uchumi unatarajiwa kuendelea kukua kutokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea kwenye miundombinu wezeshi ya uzalishaji mali kama vile barabara, madaraja, bomba la mafuta, ujenzi wa reli kwa kiwango cha kimataifa na viwanja vya ndege; Ujenzi wa kituo cha kufua umeme utokanao na nguvu za maji katika mto Rufiji chenye uwezo wa kuzalisha 2,100MW kwa ajili ya matumizi ya majumbani na viwandani; na Maboresho katika sekta ya madini na kilimo; na uanzishwaji wa kanda maalum za kiuchumi (EPZ/SEZ).

Tunatarajia pia kuwa viwanda vilivyojengwa na vitakavyojengwa vitachangia zaidi Pato la Taifa kwa kuchochea uzalishaji mali hasa bidhaa za kilimo na kuongeza thamani ya bidhaa. Aidha, mapato ya ndani yanatarajiwa kuongezeka kutokana na hatua mbalimbali za Serikali kukuza uchumi na kupanua wigo wa mapato.

Pia, maboresho ya mazingira ya biashara na uwekezaji yanayoendelea kutekelezwa na Serikali yanatarajiwa kushawishi na kuongeza ushiriki wa sekta binafsi katika uchumi na hivyo kutoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi.

Mfumuko wa bei unatarajia kuendelea kubakia katika wigo wa tarakimu moja isiyozidi asilimia 5.0 katika kipindi cha muda wa kati. Thamani ya shilingi ya Tanzania inatarajiwa pia kubaki kuwa imara.

Nakisi ya urari wa biashara ya nje inatarajiwa kupungua kufuatia mikakati ya kuongeza thamani na mauzo ya mazao ya kilimo na madini kwa kutumia viwanda vya ndani, na kuimarika kwa shughuli za utalii na huduma za usafirishaji kwenda nchi jirani.

Akiba ya fedha za kigeni itaendelea kuwa ya kuridhisha na kutosheleza mahitaji ya fedha za kigeni na kwa kiwango cha kutosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kwa miezi 4.5 kilichowekwa kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Sekta ya kibenki unatarajiwa kuendelea kuwa imara ikiwa na mitaji na ukwasi wa kutosha. Aidha, ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi unatarajiwa kuendelea kuongezeka kufuatia hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na BoT na Serikali ikiwamo kuboresha masoko ya fedha, usimamizi wa karibu wa utendaji wa mabenki, na kuboresha mazingira ya kufanya biashara.

  1. Changamoto Katika Nusu ya Pili ya 2018/19

Pamoja na kukua kwa uchumi na matarajio ya kuimarika kwa ukuaji, zipo changamoto mbalimbali ambazo zinaweza kuathiri mwenendo wa Uchumi wa Taifa na utekelezaji wa bajeti ya 2018/19 kama ifuatavyo:

  1. Kuongezeka kwa gharama za mikopo kwenye masoko ya fedha duniani kutokana na mabadiliko ya sera za fedha katika nchi kubwa kiuchumi (hususan Marekani na nchi za Ulaya) na kupungua kwa misaada ya kibajeti na fedha za washirika wa maendeleo za kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo: Katika kukabiliana na changamoto hii, Serikali inaongeza nguvu kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani na kupanua wigo na vilevile kuimarisha usimamizi wa matumizi ya Serikali. Aidha, Serikali inatafuta vyanzo vingine vya mikopo ya nje vyenye masharti nafuu katika nchi za Mashariki ya Kati na Mashariki ya mbali.
  1. Mabadiliko ya hali ya hewa yanaweza kuathiri uzalishaji hususan katika sekta mama ya kilimo ambapo sehemu kubwa bado tunategemea mvua. Mkakati wa Serikali ni kuongeza nguvu kuimarisha kilimo cha umwagiliaji, kuhifadhi vyanzo vya maji, kuhimiza matumizi ya mbegu bora za mazao ikiwa pamoja na yanayohimili ukame, na kuongeza jitihada za kutafuta masoko ya uhakika ya mazao.
  • Mvutano wa kiuchumi baina ya Marekani na China unaopelekea nchi hizo kuwekeana kodi za kulipizana kisasi (retaliatory tariffs) unaweza kuathiri biashara kati ya Tanzania na China kutokana na uwezekano wa kuongezeka kwa bei ya bidhaa tunazoagiza kutoka China. Ili kujihami, Serikali imejielekeza kupanua wigo wa bidhaa na huduma tunazouza nje (hasa utalii) na nchi washirika wa biashara.
  1. Uwezekano wa kupanda kwa bei za mafuta kwenye soko la dunia kutokana na Marekani kuiwekea tena vikwazo nchi ya Iran na vita vinavyoendelea Syria, na Yemen. Mkakati wa Serikali kukabiliana na changamoto hiyo ni kuongeza uzalishaji wa umeme kutokana na gesi asilia na vyanzo vingine mbadala, pamoja na ujenzi wa bwawa na mtambo wa kufua umeme Mto Rufiji.
  1. Hitimisho

Watanzania tumeshuhudia mafanikio makubwa sana katika kipindi cha miaka mitatu ya utawala wa Mhe. Dkt. John P.J. Magufuli. Naungana na Rais wetu kuwashukuru wananchi wote wazalendo ambao wametekeleza wajibu wao wa msingi wa kulipa kodi na kuiwezesha Serikali kugharamia miradi ya maendeleo na kupata mafanikio ya kishindo! Hakika Watanzania tunaweza.

Hata hivyo, ni dhahiri pia kuwa tumeingia katika vita kubwa ya kiuchumi (ndani na nje ya nchi). Marekebisho ya sheria na mapitio ya mikataba mbalimbali ambayo yamefanyika chini ya uongozi shupavu wa Rais Magufuli kwa lengo la kuhakikisha kuwa Watanzania wote wananufaika na rasilimali za Taifa, na pia hatua za kijasiri za kupambana na rushwa, kukusanya mapato ya Serikali na kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma, yamewaumiza wachache waliokuwa wananufaika na mfumo uliokuwepo juu ya migongo wa wananchi wanyonge.

Ninawasihi sana Watanzania wenzangu tusimame pamoja katika vita hii. Mambo matatu muhimu sana ni kuwa: (i) kila mmoja wetu awajibike kufanya kazi kwa bidii (yaani shughuli yoyote halali katika kilimo, ufugaji, uvuvi, viwandani, biashara, huduma, utumishi wa umma, na masomoni) ili kujipatia kipato au ujuzi kuwezesha kuboresha maisha yake na familia yake na pia kuchangia katika kukuza uchumi wa Taifa; (ii) kila Mtanzania mwenye kipato, awajibike na aone fahari kulipa kodi inayowiana na kipato chake ili kujijengea uhalali wa kuidai Serikali nayo kutoa huduma bora kwa wananchi. Wakati umefika kwa Tanzania kuachana na bajeti tegemezi, maana utegemezi unadhalilisha na pia unahatarisha uhuru wa kweli wa Taifa letu; na (iii) wale waliokuwa wanafaidi juu ya migongo ya Watanzania masikini, wabadilike (waokoke!) maana Watanzania wengi hawako tayari kurudi nyuma!

Kwa upande wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) napenda kuwasisitiza tena watumishi wote wa TRA kutoza kodi kwa mujibu wa sheria za kodi na kanuni zake. Kama maandiko matakatifu yanavyoelekeza: “Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa” (Luka 3:11-16). Makadirio ya kodi yasiwe kandamizi. Aidha, ninaukumbusha uongozi wa TRA utekeleze maagizo ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa katika ufunguzi wa kikao cha kazi cha TRA kilichofanyika Mwalimu Nyerere Convention Centre tarehe 10 Disemba 2018. Utaratibu wa kumfungia mfanyabiashara biashara yake ili kushinikiza alipe kodi anayodaiwa, sasa usitishwe isipokuwa kwa mkwepa kodi sugu na kwa kibali cha Kamishna Mkuu wa TRA! Badala yake, TRA ijikite zaidi kutoa elimu kwa mlipa kodi juu ya utunzaji wa vitabu vya hesabu za biashara, na kumpa fursa ya kufanya naye majadiliano kuhusu mpangilio bora wa kulipa malimbikizo ya kodi kwa mkupuo au kwa awamu pamoja na adhabu stahiki kama zilivyobainishwa kwenye Sheria ya Usimamizi wa Kodi 2015. Matumizi ya lugha mbaya, vitisho na ubabe dhidi ya walipa kodi wenye historia nzuri ya kulipa kodi stahiki yasipewe nafasi kabisa, na pale inapothibitika kwenda kinyume na maadili mema basi mtumishi husika awajibishwe mara moja kwa kuzingatia taratibu za kiutumishi. Vilevile, mtumishi wa TRA yeyote anayetuhumiwa kupokea au kudai rushwa asimamishwe kazi mara moja kupisha uchunguzi wa vyombo husika (TAKUKURU na Jeshi la Polisi). Aidha ninaiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania kuongeza jitihada za kudhibiti biashara ya magendo inayoendeshwa na wafanyabiashara wanaopitisha mizigo bandari bubu kwa nia ya kukwepa kodi hususan eneo la mwambao wa bahari ya Hindi na sehemu zote za mipakani na kuhakikisha kodi stahiki inalipwa mara moja na bidhaa zilizokamatwa kutaifishwa.

Kwa upande wa mabenki, Serikali inayataka mabenki yote ya biashara nchini yaongeze jitihada za kupeleka huduma za kibenki vijijini katika mwaka ujao 2019, kwa kuanza na shughuli na maeneo ambayo yana fursa za kupanua wigo wa huduma za kibenki kama vile minada ya mifugo, masoko makubwa mipakani na miji midogo na ile inayoibukia kibiashara.

Napenda kuwahakikishia tena wafanyabiashara kuwa Serikali inathamini sana mchango adhimu wa wafanyabiashara katika maendeleo ya Taifa hili. Serikali imedhamiria kuongeza jitihada kurahisisha mazingira ya kufanya biashara nchini na hususan kwa kupitia tena mfumo wa kodi na tozo mbalimbali zinazowakwaza. Aidha, katika kipindi kilichobaki cha mwaka wa fedha 2018/19, Serikali itaongeza kasi ya kulipa madeni na madai mbalimbali kwa serikali yaliyohakikiwa. Lengo letu ni kumaliza kulipa madai mbalimbali kwa muda tuliojiwekea kwenye mkakati wa kulipa madai halali na kudhibiti malimbikizo mapya. Hata hivyo, Serikali inaendelea kuwakumbusha wafanyabiashara wema kulipa kodi kwa mujibu wa sheria ili kuchangia ujenzi wa nchi yao. Ukwepaji kodi hauna nafasi chini ya Serikali ya awamu ya tano.

Kwa mara nyingine napenda, kwa niaba ya Serikali, kuwapongeza sana wakulima, wafugaji, wavuvi, wafanyakazi viwandani, sekta binafsi kwa ujumla, watoa huduma na watumishi wa umma waliofanya kazi kwa bidii katika nusu ya kwanza ya 2018/19 na kuufanya uchumi wetu kuendelee kukua kwa kasi na pia kwa kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi. Aidha, ninawakumbusha wananchi wote agizo la Mheshimiwa Rais kwamba “UKIUZA, TOA RISITI. UKINUNUA DAI RISITI”

Mwisho kabisa ninawaalika wadau wote wa kodi na wananchi kwa ujumla kutuletea kwa maandishi mapendekezo na ushauri kuhusu vyanzo vipya vya mapato ya Serikali na marekebisho ya viwango vya kodi kwa ajili ya bajeti ya Serikali kwa mwaka ujao wa fedha 2019/20 na ninaomba mapendekezo hayo yawasilishwe kwa maandishi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango kabla ya tarehe 10 Februari 2019.

Nawatakia Wazalendo wote wa Watanzania HERI YA MWAKA MPYA 2019.

Ad

Unaweza kuangalia pia

LIVE: UZINDUZI WA MAJENGO YA OFISI YA MANISPAA NA MKUU WA WILAYA KIGAMBONI JIJINI DSM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 11, Febuari, …

Leave a Reply to Festo Mwaniloli Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *