RAIS MAGUFULI ATAKA WATANZANIA KUJIVUNIA MAFANIKIO YA NCHI YAO

  • Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amesema Watanzania wana kila sababu ya kutangaza na kujivunia mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi kifupi cha miaka minne iliyopita na ameahidi kuendelea kusimamia rasilimali za Taifa ili ziwanufaishe zaidi.
1-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwahutubia wananchi katika mkutano uliofanyika katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi.
  • Mhe. Rais Magufuli ameyasema hayo leo tarehe 10 Oktoba, 2019 wakati akihutubia wananchi wa Mkoa wa Katavi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Azimio Mjini Mpanda.
2-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwahutubia wananchi katika mkutano uliofanyika katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi.
  • Amesema juhudi kubwa zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kubana mianya ya wizi, ufisadi, rushwa, matumizi mabaya ya ofisi na mali za umma na kudhibiti nidhamu kwa watumishi wa umma zimesaidia kuokoa fedha nyingi ambazo zimetumika kutekeleza miradi mingi ya maendeleo ikiwemo ile ambayo ilionekana kutowezekana.
3-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wananchi wa Mpanda mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi kwa ajili ya kuwahutubia.
  • Rais Magufuli ametaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni ujenzi wa Bwawa la kuzalisha umeme la Nyerere ambao utagharimu shilingi Trilioni 6.5, ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (standard gauge railway – SGR) utakaogharimu shilingi Trilioni 7.2, ununuzi wa ndege, ujenzi wa barabara na madaraja makubwa, ujenzi wa vituo vya afya na Hospitali za Wilaya, ujenzi wa miundombinu ya elimu na kutoa shilingi Bilioni 23.8 kila mwezi kwa ajili ya kugharamia elimu bila malipo kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.
5-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wananchi wa Mpanda mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi kwa ajili ya kuwahutubia.
  • “Ni lazima tujiulize maswali sisi Watanzania bila uoga na bila kumuonea mtu, kama tumeongeza ukusanyaji mapato kutoka Bilioni 850 hadi Trilioni 1.3 na mwezi uliopita tumekusanya shilingi Trilioni 1.7, kama tumejenga Vituo vya Afya 352 kwa mpigo, tumejenga Hospitali za Wilaya 69 wakati tangu tupate uhuru tulikuwa na Hospitali za Wilaya 77 tu, hela hizo zilikuwa zinakwenda wapi? Ukweli unabaki palepale, kama tumenunua ndege na sasa zitakuwa 11 kwa nini hatukununua miaka 50 iliyopita? Nyerere alipoondoka aliacha ndege, zote zimepotea, zipo wapi? Hilo nalo ukisema ni nongwa ndugu zangu, ukitaka kupima maendeleo ni lazima ujue mahali ulipotoka, mahali ulipo na mahali unapokwenda, hicho ndicho kipimo cha maendeleo cha kila mtu, treni ilikua inakufa mpaka tukabinafsisha kwa watu wengine, hapa Mpanda mlikuwa hamuoni treni, leo treni inakuja, ndugu zangu mnasahau? Amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
6-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wananchi wa Mpanda mara baada ya kuwasili katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi kwa ajili ya kuwahutubia.
  • Amewataka viongozi wote wa Serikali, siasa, Dini na taasisi binafsi kuyatangaza mafanikio hayo makubwa ili Watanzania wajue nchi yao inakokwenda na wapate moyo zaidi wa kuendelea kuijenga kwa kuchapa kazi kwa juhudi na maarifa.
  • Mhe. Rais Magufuli amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Juma Homera kwa juhudi kubwa alizozifanya kusimamia maendeleo ya Mkoa huo katika kipindi kifupi cha miezi 4 tangu ateuliwe kuongoza Mkoa huo ambapo amefanikiwa kusimamia uanzishaji wa soko la madini na hivyo kuongeza ukusanyaji wa mapato kutoka shilingi laki 6 kwa mwezi hadi kufikia shilingi Milioni 148, kusimamia masoko ya mazao ya tumbaku, pamba na mahindi, kutatua kero za wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi na mkakati wa kuanzisha viwanda.
7-01
Wanakwaya ya Agape wakitumbuiza katika uwanja wa Azimio Mpanda mkoani Katavi mara baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwasili uwanjani hapo
  • Rais Magufuli ameahidi kuwa Serikali itatoa fedha za kujenga kiwanda cha kuchambua pamba (Ginnery) katika Mkoa wa Katavi ambacho kitagharimu shilingi Bilioni 1.6 lakini amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Katavi na Wizara ya Kilimo kuhakikisha wakulima wa pamba ambao hawajapata malipo ya kilo Milioni 6 za pamba wanalipwa ndani ya siku 7.
  • Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameiagiza Wizara ya Maji na Mkoa wa Katavi kufuatilia miradi ya maji ambayo utekelezaji wake unasuasua Mkoani humo ikiwemo miradi 9 yenye thamani ya shilingi Bilioni 3.109.
8-01
Kwaya ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mpanda Girls wakitumbuiza mara baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwasili uwanjani hapo.
  • Rais Magufuli ameelezea kusikitishwa na taarifa baadhi ya wakimbizi wa kutoka nchi jirani wanaodaiwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu Mkoani Katavi na ametoa wito kwa wakimbizi hao kuacha vitendo hivyo na Vyombo vya Dola kuhakikisha uhalifu huo unakomeshwa.
  • Kabla ya mkutano huo, Mhe. Rais Magufuli amefungua barabara ya lami ya Sitalike – Mpanda yenye urefu wa kilometa 36.9 ambayo imegharimu shilingi Bilioni 39.8 (fedha zote zimetolewa na Serikali ya Tanzania) na pia ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Tabora (Usesula) – Konga – Mpanda yenye urefu wa kilometa 342.9 ambayo itakapokamilika Machi 2021 itagharimu shilingi Bilioni 450.
9-01
Kwaya ya Manispaa ya Sumbawanga ikitumbuiza mara baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwasili katika uwanja wa Azimio mkoani Katavi. PICHA NA IKULU
  • Pia Mhe. Rais Magufuli amefungua Kituo Kikuu cha Mabasi cha Mkoa wa Katavi kiitwacho Mizengo Pinda, ambacho ujenzi wake umegharimu shilingi Bilioni 4.4 na amewapongeza wananchi wa Manispaa ya Mpanda kwa kupata kituo hicho pamoja na kujengewa barabara mpya za Mjini zenye urefu wa kilometa 7.7 kwa gharama ya shilingi Bilioni 8 hali inayoufanya Mji huo kuwa nadhifu.
  • Kesho tarehe 11 Oktoba, 2019 Mhe. Rais Magufuli ambaye ameongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli ataendelea na ziara yake Mkoani Katavi ambapo ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilowati 132 kutoka Tabora kwenda Mpanda, ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika na ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Mpanda – Vikonge.
Ad

Unaweza kuangalia pia

LIVE: UZINDUZI WA MAJENGO YA OFISI YA MANISPAA NA MKUU WA WILAYA KIGAMBONI JIJINI DSM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 11, Febuari, …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *