SERIKALI YAOKOA ZAIDI YA SH. BILION 89 KWA WAGONJWA 5954 WALIOFANYIWA UPASUAJI WA KUFUNGUA NA BILA KUFUNGUA KIFUA KATIKA TAASISI YA MOYO (JKCI)

  • Kwa kipindi cha miaka minne Serikali imeweza kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 89 kwa wagonjwa 5954 wenye matatizo makubwa ya moyo ambao walifanyiwa  upasuaji wa kufungua na bila kufungua kifua katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
  • Kama wagonjwa hawa 5954 waliofanyiwa upasuaji hapa nchini wangetibiwa nje ya nchi Serikali ingetumia zaidi ya shilingi  bilioni 178 kulipia gharama za matibabu hayo.
3-01
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi zawadi ya ngao mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya Taasisi hiyo Prof. William Mahalu kama ishara ya kutambua na kuthamini kazi aliyoifanya kwa kipindi cha miaka mitatu ya kuongoza bodi hiyo ambayo imemaliza muda wake tarehe 13/11/2019.
  • Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi wakati akielezea mafanikio  ya miaka minne ya Serikali ya awamu ya tano kwa upande wa matibabu ya moyo katika kikao cha bodi ya wadhamani ya Taasisi hiyo.
  • Prof. Janabi alisema kwa wagonjwa hao kutibiwa hapa nchini matibabu yao yamegharimu kiasi cha shilingi bilioni 89 fedha ambazo zimelipwa kupitia bima zao za matibu, misaada ya wafadhili mbalimbali wa nje, wagonjwa wenyewe kujilipia na Serikali kugharamia matibabu ya wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za matibabu.
4-1-01
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi zawadi ya ngao mjumbe wa bodi ya wadhamini ya JKCI Dkt. Donan Mmbando kama ishara ya kutambua na kuthamini kazi aliyoifanya kwa kipindi cha miaka mitatu kama mjumbe wa bodi hiyo ambayo imemaliza muda wake tarehe 13/11/2019.
  • “Gharama ya mgonjwa mmoja aliyefanyiwa upasuaji  nje ya nchi ni zaidi ya shilingi milioni 30, lakini kwa mgonjwa mmoja  kutibiwa hapa nchini gharama zake hazizidi shilingi milioni 15. Kwa kutibiwa hapa nchini fedha anazolipa mgonjwa zinatumika kununua  vifaa tunavyomuwekea  katika moyo wake  kama vile pacemaker, high power device, stent, device closure   na  valvu vifaa hivi tunaviagiza  nje ya nchi kwani hazipatikani hapa nchini”, alisema Prof. Janabi.
  • Mkurugenzi huyo Mtendaji aliendelea kusema kwa kipindi cha miaka minne wameweza kuona wagonjwa 300,836 kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani pamoja na nchi jirani kama vile Demokrasia ya Congo, Malawi, Ethiopia, Zambia, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda na Visiwa vya Comoro.
5-01
Mjumbe wa Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Lawrence Museru ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) akizungumza katika kikao cha bodi hiyo kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam huku Dkt. Donan Mmbando akimsikiliza kwa makini.
  • “Jambo la kufurahia ni kuwa tumeweza kuokoa maisha ya watu ambao tumewatibu na hivi sasa wanaendelea na majukumu yao ya kazi za kila siku. Kwa kipindi cha miaka minne tulilaza wagonjwa 14,960 tumefanya upasuaji wa bila kufungua kifua kwa kutumia  mtambo wa Cathlab kwa wagonjwa 4,207 na upasuaji wa kufungua kifua na kusimamisha moyo kwa wagonjwa 1,747”,alisema Prof. Janabi.
  • Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo ambayo inamaliza muda wake Prof. William Mahalu aliupongeza uongozi wa Taasisi hiyo pamoja na wafanyakazi kutokana na huduma za matibabu ya moyo wanazozitoa kwa wagonjwa wanaowatibu.
7-01
Mjumbe wa Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Andrea Pembe ambaye pia ni mkuu wa chuo kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) akizungumza katika kikao cha bodi hiyo kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam. Kulia ni mjumbe wa bodi hiyo CPA Godfrey Kirenga.
  • Prof. Mahalu ambaye ni mmoja wa madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa kwanza hapa nchini alisema anamaliza muda wake kama Mwenyekiti wa bodi  hiyo huku ndoto yake ya kuona Tanzania inakuwa na Hospitali ya  matibabu ya moyo ikiwa imetimia.
  • “Ninamshukuru sana Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniteua kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini ya Taasisi hii kwa kipindi cha miaka mitatu. Kama mtakumbuka tangu nchi yetu ipate Uhuru mwaka 1961 wananchi wengi wenye matatizo ya moyo yaliyohitaji kufanyiwa matibabu ya kibingwa iliwalazimu kwenda kutibiwa nje ya nchi.
1-01
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akielezea mafanikio ya miaka minne ya Serikali ya awamu ya tano kwa upande wa matibabu ya moyo katika kikao cha cha bodi ya wadhamani ya Taasisi hiyo kiichofanyika jana jijini Dar es Salaam.
  • “Kwa kuwa kutibiwa nje ya nchi ni gharama na pia mlolongo kuwa mrefu baadhi ya wagonjwa walipoteza maisha wakati wakisubiri fedha za  kwenda kupata matibabu. Hivi sasa wananchi hawapati tabu tena wanatibiwa hapa nchini kwa wakati. Ukiangalia idadi ya wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi yetu imeongezeka kutoka wagonjwa 150 kwa mwaka 2016 hadi kufikia wagonjwa 300 kwa siku kwa mwaka 2019”, alisema Prof. Mahalu.
  • Prof. Mahalu alisema wakati anasomea upasuaji wa moyo nje ya nchi kuna daktari alimkatisha tamaa na kumwambia kuwa hawataweza lakini hakukata tamaa alihakikisha anasoma kwa bidii na baada ya kuhitimu masomo yake aliweza kufanya upasuaji na alimualika yule daktari aliyemkatisha tamaa kwenda kushuhudia jinsi wanavyofanya upasuaji.
2-01
Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu akizungumza na wajumbe wa bodi ya wadhanini pamoja na menejimenti ya Taasisi hiyo katika kikao cha mwisho cha bodi hiyo kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam.
  • Aidha Prof. Mahali aliwashukuru wajumbe wa Bodi ya wadhamini kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuhakikisha Taasisi ya Moyo inafanya kazi zake za kutoa huduma kwa wananchi kwa weledi na wakati.
  • Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo ambayo imemaliza muda wake jana tarehe 13/11/2019 kwa kufanya kazi kwa kipindi cha miaka mitatu ilizinduliwa na Mhe. Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto  Mhe. Ummy Mwalimu  tarehe 21 Machi 2017.
Ad

Unaweza kuangalia pia

ONGEZENI KASI YA KUWAHUDUMIA WANANCHI – DKT. CHAULA

Watumishi wa afya nchini wametakiwa kuongeza kasi ya kuwahudumia wananchi kwenye vituo vya kutolea huduma …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *