Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa amesema mradi wa kufua Umeme kwa kutumia Maji wa Julius Nyerere ni mradi mkubwa na ni mradi wa kimkakati.
Waziri Mkuu amesema hayo katika hafla ya uzinduzi rasmi wa njia ya mchepuko kupitisha maji kwenye mradi wa umeme wa Julius Nyerere, ambapo uzinduzi huo umefanyika leo tarehe 18 Novemba, 2020 kwenye eneo la mradi lililopo mto Rufiji mkoani Pwani.
Waziri Mkuu amesema kuwa mradi huo ni wa aina yake katika Ukanda wa Afrika ukiwa ni wa kwanza kwa ukubwa kwa Afrika Mashariki na Nchi za Jumuiya ya maendeleo Kusini mwa Afrika(SADC) na wanne katika Bara la Afrika
“Nimeambiwa kuwa mradi huu unaenda sambamba na ujenzi wa njia ya kusafirishia umeme wa msongo kilovoti 400 itakayotoka hapa na kuelekea eneo la Chalinze ili kuweza kuusambaza kwa njia za Morogoro, Dodoma, Iringa mpaka Mbeya lakini pia kuanzaia Chalinze kwenda Segera mpaka, Manyara, Moshi na Arusha ili kuhakikisha umeme usambaa kote na kuingizwa kwenye grid ya Taifa” – Waziri Mkuu Majaliwa
Pia Waziri Mkuu Majaliwa amepata nafasi ya kutembelea na kukagua ujenzi w jengo la Stesheni ya Reli ya Kisasa – SGR mkoani Morogoro na kusema kuwa ameridhishwa na kasi ya maendeleo ya Mradi wa SGR.