Rais Dkt. John Magufuli leo tarehe 11 Desemba, 2020 amemuapisha Prof. Shukrani E. Manya kuwa Naibu Waziri wa Madini.
Hafla ya kuapishwa kwa Prof. Manya imefanyika Ikulu, Chamwino Mkoani Dodoma na kuhudhuriwa na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yustino Ndugai, Waziri wa Madini Doto Mashaka Biteko, Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi John Kijazi, Makatibu Wakuu, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama na wafanyakazi wa Wizara ya Madini.
Prof. Manya pia amekula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma kilichoongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma Mhe. Latifa Mansour.
Akizungumza baada ya kumuapisha, Rais Magufuli amemtaka Prof. Manya kutumia taaluma yake vizuri katika kuhakikisha Watanzania wananufaika na rasilimali yao ya madini badala ya kuacha rasilimali hiyo ikihujumiwa kwa utoroshaji, wizi, ukwepaji kodi na kuingia mikataba isiyofaa.
Amemtaka kwenda kushirikiana na viongozi wenzake wakiwemo Waziri, Katibu Mkuu na Wataalamu wa Wizara kuhakikisha wanafanya uamuzi na kukwamua masuala ambayo yalikuwa yamekwama kwa muda mrefu ili sekta ya madini ambayo imefanikiwa kuongeza mapato kutoka shilingi Bilioni 168 mwaka 2015 hadi kufikia shilingi Bilioni 527 iongeze mapato zaidi.
Rais Magufuli ametoa wito kwa Wizara ya Madini kujadiliana na wadau ili madini yaliyopo nchini yatumike kuzalisha bidhaa mbalimbali ikiwemo chuma badala ya kutegema vyuma chakavu ambavyo baadhi huibwa kutoka kwenye miradi ya ujenzi wa reli au kuingizwa nchini kutoka nchi za nje, na kuzalisha umeme kwa kutumia urani na makaa ya mawe.
Aidha, Rais Magufuli ameagiza waliokuwa wafanyakazi wa Wakala wa Ukaguzi wa Madini (TMA) na ambao walihamishiwa Wizara ya Madini kupunguziwa mishahara ili iendane na viwango vya mishahara vya watumishi wa Wizara hiyo.
Rais Magufuli amesema wafanyakazi hao hawawezi kuendelea kulipwa mishahara mikubwa kuwazidi viongozi wao wa wizara hasa baada ya ofisi waliyokuwa wameajiriwa kuvunjwa kutokana na utendaji usioridhisha.
“Nataka wafanyakazi wote wa iliyokuwa TMAA wapunguziwe mishahara, na ambaye ataona mshahara hautoshi aondoke” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Rais Magufuli amewataka Watanzania wote waendelea kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuitikia maombi yao ya kuliepusha Taifa dhidi ya ugonjwa wa Korona (Covid–19) ambao unaendelea kuangamisha maisha ya maelfu ya watu katika nchi mbalimbali duniani ilihali Tanzania ikiwa shwari.