RAIS SAMIA ATOA WITO KWA WATANZANIA KUTUNZA VYANZO VYA MAJI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Maji Safi na usafi wa Mazingira  (DAWASA) Mhandisi Cyprian Luhemeja wakati akielezea kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji katika Mkoa wa Dar es Salam kwenye Maadhimisho ya kilele cha Wiki ya Maji  iliyofanyika Mlimani City Jijini Dar es Salaam leo tarehe 22 Machi 2022.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuzindua Taarifa ya mwaka ya Utendaji Kazi wa Mamlaka za maji na mazingira mijini kabla ya kuzungumza na viongozi mbalimbali katika maadhimisho ya kilele cha Wiki ya Maji iliyofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Ad

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali katika kilele cha Wiki ya Maji iliyofanyika Mlimani City Jijini Dar es Salaam leo tarehe 22 Machi 2022.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ametoa wito kwa Watanzania kutunza mazingira, hususan uoto wa asili kwa kuepuka kukata au kuchoma miti ovyo.

Mhe. Rais ametoa wito huo leo wakati akihutubia katika Kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Maji kilichofanyika katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Rais Samia amesema katika maeneo ya vijijini, chemichemi nyingi za maji pamoja na baadhi ya mito imetoweka kutokana na uharibifu wa mazingira, na pia kutokana na kufanya shughuli nyingine za kibinadamu karibu na vyanzo vya maji.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo kutoka kwa Mhandisi Judith Odunga kwa niaba ya Chama cha Wahandisi Wanawake Tanzania ya kutambua mchango wake katika utendaji wake wa kazi kwenye sekta ya maji nchini.

Aidha, Rais Samia ameielekeza Wizara ya Maji kufanya utafiti na kuangalia uwezekano wa kutumia maji ya Mto Rufiji kwa ajili ya matumizi ya baadae katika jiji la Dar es Salaam.

Awali akizindua mradi wa maji uliogharimu shilingi Bilioni 18 utakaosambaza maji kutoka Mboga, Chalinze hadi Mlandizi Wilayani Bagamoyo, Rais Samia ameikopesha Wizara ya Maji shilingi Milioni 500 kwa ajili ya kusambaza maji kwa wananchi ili yaweze kuwafikia kwa haraka.

Pia, Mhe. Rais Samia amewataka wananchi kuhakikisha wanalipa ankara za huduma ya maji wanayopatiwa ili Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira mkoani Dar es Salaam (DAWASA) iendelee kutoa huduma kwao.

Vile vile, Rais Samia amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Pwani kuweka mikakati ya kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza Mkoani humo kwa kuhakikisha kuwa wanatenga maeneo maalum kwa ajili ya uwekezaji.

Wakati huo huo, Rais Samia amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Mfalme wa Saudi Arabia Mhe. Ahmed Abdulazizi Kattan Ikulu Jijini Dar es Salaam ambapo wamezungumzia kuendelea kuimarisha uhusiano uliopo kati ya nchi hizo mbili hususan katika masuala ya uwekezaji.

Ad

Unaweza kuangalia pia

BANDARI YA DAR ES SALAAM INAPANUKA NA KUIMARIKA: HATUA MUHIMU KWA UCHUMI WA TANZANIA

Bandari ya Dar es Salaam ni kitovu muhimu cha biashara na uchumi wa Tanzania, na …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *