Serikali Yaandaa Mpango wa Mageuzi ya Sekta ya Mifugo ili Kukuza Ufugaji wa Kisasa Nchini

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, amesema kuwa Serikali imeandaa mpango wa mageuzi ya sekta ya mifugo ambao utasaidia kupunguza changamoto zinazokabili sekta hiyo nchini. Dkt. Biteko alitoa wito kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kubuni mbinu na mikakati ya kuondokana na ufugaji usio na tija na kuwezesha ufugaji wa kisasa.

Dkt. Biteko alisema hayo Kibaha, Pwani, tarehe 16 Juni 2024, wakati akifunga Maonesho na Mnada wa Mifugo kwa mwaka 2024. Alisisitiza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi inapaswa kuendelea kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu ufugaji wa kisasa ili kuboresha uzalishaji. Alisema, “Lazima tukubali kuwa mabadiliko ni muhimu na maeneo mengi yanayohitaji ardhi yanaongezeka huku ardhi yenyewe ikibaki ile ile. Hivyo, tuendelee kuwapa elimu ya ufugaji wa kisasa na kuwahimiza wafugaji kuhudhuria maonesho kama haya ili wapate ujuzi na teknolojia itakayowasaidia.”

Ad

Dkt. Biteko aliongeza kuwa ni muhimu kwa wafugaji kutambua mabadiliko yanayotokea duniani na kujiandaa kwa hayo mabadiliko ili kufuga kwa tija zaidi. Alisema, “Wafugaji lazima waone ufugaji kama mtaji mkubwa wa kubadilisha maisha yao. Mfugaji mwenye ng’ombe 1,000 anaweza kujiinua kiuchumi ikiwa atatumia rasilimali hizo kwa busara.”

Pia, Dkt. Biteko alieleza kuwa Serikali imefanya jitihada mbalimbali kuboresha sekta ya mifugo, ikiwemo kutenga maeneo maalum kwa ajili ya malisho ya mifugo. Aliwaasa wafugaji kuepuka migogoro na wakulima kwa sababu wanategemeana na migogoro hiyo ina athari za kijamii na kiuchumi.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko alipendekeza maonesho ya mifugo yafanyike kikanda ili kuwafikia wakulima wengi zaidi na kusaidia kupata ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili, kama vile mbegu bora za mifugo na teknolojia za kisasa za ufugaji.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Alexander Mnyeti, aliongeza kuwa maonesho hayo ni muhimu kwa kuwa yanatoa elimu kwa wafugaji ili kuongeza tija. Alisema, “Maonesho haya yanaleta matokeo makubwa na tunajitahidi kuwahamasisha wafugaji wetu kufuga kisasa badala ya kizamani. Tunatoa elimu kupitia wataalamu na Maafisa Ugani, ingawa bado kuna mwamko mdogo wa kufuga kisasa.”

Mhe. Mnyeti alisisitiza umuhimu wa elimu ya ufugaji wa kisasa, akitaja faida za kunenepesha mifugo ili kuongeza thamani yake sokoni. Alisema, “Wafugaji lazima wajue kuwa ng’ombe ambaye hajafugwa kisasa na hajapata chanjo hawezi kuuzwa nje ya nchi kwa sababu hana ubora.”

#NA HAYA NDIYO MATOKEO CHANYA+

Ad

Unaweza kuangalia pia

AMKA TANZANIA, KAZI NI MAENDELEO, TUIJENGE NCHI YETU.

SIO NDOTO TENA!! TUKIISHI FALSAFA YA 4R YA RAIS DKT SAMIA TUTAJENGA TAIFA IMARA NA …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *