- Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza kuwa ardhi iliyotengwa kwa ajili ya kilimo hapa Zanzibar ni vyema ikatumika kwa ajili ya shughuli hiyo na si vyenginevyo.
- Rais Dk. Shein aliyasema hayo katika hotuba yake aliyoitoa katika uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji huko Kinyasini Kisongoni, Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
- Alieleza kuwa kilimo ni ardhi, hivyo endapo ardhi haitokuwepo kilimo hakitofanyika kwani hata historia ya Zanzibar inaonesha wafanyakazi na wakulima walishindwa kulima kabla ya Mapinduzi kutokana na kunyanganywa ardhi yao.
- Rais Dk. Shein alisema kuwa hapa Zanzibar hivi sasa ardhi imekuwa ndogo sana kutokana na matumizi mabaya ya ardhi yanayofanywa na baadhi ya wananchi.
- Akieleza historia ya ardhi, Rais Dk. Shein alisema kuwa miaka mingi kabla ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 Wazanzibari waliteseka katika kutafuta ardhi na pale walipotaka kulima ilibidi wakapige magoti kwa wakoloni.
- Alisema kuwa madhila ya kunyanyaswa katika ardhi yao yaliondoshwa na Mapinduzi yaliyomg’oa Sultani mnamo Januari 12, 1964 ambapo ni miaka 56 tokea kutokea Mapinduzi hayo.
- Alisema kuwa uhuru wa Zanzibar unahisabika rasmi kuanzia Januari 12, 1964 na kupelekea sekta zote ikiwemo ardhi kuwa huru na tarehe 8 Machi 1964 hayati mzee Karume alitoa tangazo rasmi la SMZ ikiwa ni amri na sheria ya Serikali ambayo ilitengenezwa utaratibu wa sheria na katiba juu ya sekta hizo ikiwemo ardhi.
Ad