Rais Magufuli aishukuru Kuwait kwa kutoa Bilioni 110 za barabara ya Nyahua – Chaya

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ameishukuru Serikali ya Kuwait kwa kutoa mkopo wa Dola za Marekani Milioni 51 sawa na takribani Shilingi Bilioni 110 kwa ajili ya kujenga barabara ya Chaya – Nyahua Mkoani Tabora yenye urefu wa kilometa 85 ambayo itaunganisha mawasiliano ya barabara kati ya mkoa wa Singida na Tabora.

Mhe. Rais Magufuli ametoa shukrani hizo leo tarehe 05 Juni, 2017 Ikulu Jijini Dar es Salaam alipofanya mazungumzo na Balozi wa Kuwait hapa nchini Mhe. Jasem Ibrahim Al Najem na kupokea msaada wa magari mawili ya kusombea taka ngumu yenye thamani ya Dola za Marekani 200,000/- yaliyotolewa na Serikali ya Kuwait kwa lengo la kuunga mkono kampeni ya usafi hapa nchini.

Ad

“Naomba unifikishie salamu zangu kwa Mfalme wa Kuwait, mwambie tunathamini mchango mkubwa wa Kuwait katika maendeleo ya nchi yetu, hizi fedha za barabara mlizotupatia zitatusaidia kumalizia sehemu hiyo ya barabara ambayo ndio ilikuwa imebaki” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli pia ameishukuru Serikali ya Kuwait kwa kuunga mkono juhudi mbalimbali za utoaji wa huduma za kijamii hapa nchini ikiwemo msaada wa Dola za Marekani 250,000 kwa ajili ya kununulia vifaa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete na visima vya maji safi 27 vilivyochimbwa Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya wananfunzi na wananchi wa maeneo jirani na shule.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameishukuru Serikali ya Kuwait kwa kutoa Dola za Marekani Milioni 50 kwa ajili ya kuikarabati hospitali ya rufaa ya Mnazi Mmoja iliyopo Zanzibar.

Mhe. Rais Magufuli pia ameiomba Serikali ya Kuwait kuweka alama ya kumbukumbu ya uhusiano wake na Tanzania kwa kusaidia ujenzi wa barabara za Makao Makuu ya nchi Mjini Dodoma na amemhakikishia Mfalme wa Kuwait Sheik Sabah Al-Ahmad Al-Jaber Al-Sabah kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Kuwait hususani katika masuala ya kiuchumi ikiwemo mafuta na gesi ambayo imevumbuliwa kwa kiasi kikubwa nchini Tanzania.

Kwa upande wake Balozi wa Kuwait hapa nchini Mhe. Jasem Ibrahim Al-Najem ameelezea kufurahishwa kwake na uhusiano na ushirikiano mzuri kati ya nchi yake na Tanzania na amemhakikishia Mhe. Rais Magufuli kuwa Kuwait ipo tayari wakati wowote kuunga mkono juhudi za maendeleo kulingana na vipaumbele vya Tanzania.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amefanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambaye ni Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kongo Mhe. Leonard She Okitundu na kumhakikishia kuwa Tanzania inaunga mkono juhudi za kumaliza tofauti kati ya pande zinazopinga nchini Kongo.

Pamoja na kukabidhi barua yenye ujumbe wa Rais wa DRC Mhe. Joseph Kabila Kabange, Balozi Leonard She Okitundu amemueleza Mhe. Rais Magufuli kuwa hali ya Kongo ni shwari na kwamba mchakato wa mazungumzo kati ya pande zinazopingana nchini humo unaendelea vizuri. Katika hatua nyingine, Mhe. Rais Magufuli amefanya mazungumzo na
Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Msumbiji ambaye ni Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo Jenerali Atanasio Salvador Ntumuke. Baada ya mazungumzo hayo, Jenerali Atanasio Salvador Ntumuke amesema Msumbiji itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa mambo mbalimbali kwa kuwa nchi hizo ni ndugu na zimesaidiana kwa mengi tangu harakati za kupigania uhuru ambapo Tanzania ilitoa mchango mkubwa.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam
05 Juni, 2017

Ad

Unaweza kuangalia pia

MAKAMU WA RAIS ATEMBELEA MRADI WA MAJI SAME MWANGA KOROGWE

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akimsikiliza Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma Waziri kuhusu maendeleo ya ujenzi wa mradi wa maji Maji wa Same – Mwanga – Korogwe wakati alipotembelea chanzo cha mradi huo eneo la la Nyumba yaMungu Wilaya ya Mwanga wakati akiwa ziarani mkoani Kilimanjaro tarehe 21 Machi 2024. Makamu …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *