WAZIRI NAPE AANZA ZIARA KUKAGUA MWENENDO WA OPERESHENI ANWANI ZA MAKAZI

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye leo ameanza ziara ya kukagua na kuhamasisha utekelezaji wa Operesheni ya Anwani za Makazi katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro na Arusha

Akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kuanza ziara hiyo jijini Dodoma, Waziri Nape amesema tathmini inaonesha utekelezaji wa operesheni hiyo ni asilimia 69 huku baadhi ya maeneo yakiwa na changamoto na kutofanya vizuri akiitaja kwa mfano mikoa ya Tanga na Dar es Salaam.

Ad

“Kwa muda uliobaki tumekubaliana tuongeze nguvu kwa kutoka ofisini na kuifikia mikoa yote nchi nzima ili kukagua na kuhamasisha utekelezaji wa operesheni ya Mfumo wa Anwani za Makazi unaojumuisha ukusanyaji wa taarifa, kuweka taarifa kwenye mfumo wa kidijitali na uwekaji wa namba za nyumba, majina ya barabara na mitaa”, Amezungumza Waziri Nape.

Ameongeza kuwa, Operesheni ya anwani za makazi inalenga kuhakikisha kila mtanzania anatambulika mahali alipo, mahali anapofanyia kazi/biashara na anapoishi hivyo ushirikiano wa pamoja utaifanya nchi ya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi ambazo unaweza kupata huduma ukiwa nyumbani kwako

“Katika mazingira haya ya dunia inayokwenda kidigitali si vema kwa nchi kuachwa nyuma, tumuunge mkono Mhe. Rais Samia kwenye operesheni hii na tujitendee haki watanzania kwa kuhakikisha tunakuwa na Anwani za Makazi”, amesisitiza Waziri huyo

Aidha, katika ziara hiyo Waziri Nape ameambatana na Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo pamoja na baadhi ya wataalamu ambapo wanatumia usafiri wa helkopta ili kuifikia mikoa zaidi ya mitatu kwa siku, kwa kuwa zoezi hilo ni operesheni maalumu na Wizara imejipanga kwenda kuona mwenendo wa utekelezaji na kuongeza nguvu maeneo yenye Changamoto.

Ad

Unaweza kuangalia pia

#LIVEDAY2: JUKWAA LA KODI NA UWEKEZAJI 2024

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.