WAZIRI MAKAMBA AELEZA MAFANIKIO YA SEKTA YA NISHATI NA MIKAKATI YA KUENDELEZA SEKTA

Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba ametaja mafanikio mbalimbali ya Sekta ya Nishati yaliyofikiwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Samia Suluhu Hassan.

Mafanikio hayo aliyataja tarehe 24 Machi, 2022 wakati akizungumza na Wahariri wa Vyombo mbalimbali vya Habari na wanazuoni jijini Dar es Salaam.

Ad

Mafanikio aliyoyataja ni pamoja  na  Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuhamishiwa Wizara ya  Nishati ambapo imeimarishwa na kufanyiwa mabadiliko kadhaa ya kikanuni na kiuendeshaji yanayowezesha Taasisi hiyo kudhibiti kwa weledi sekta nyeti ya umeme na mafuta.

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) sasa umewekwa kwenye nafasi yake, kwani haujikiti  katika umeme pekee bali na nishati nyingine ikiwemo ya kupikia, mafuta na nyinginezo na kwa sasa imebuniwa miradi mingine ya nishati na hasa nishati ya kupikia ambayo ndiyo nishati namba moja hapa nchini.

Waziri wa Nishati, Mhe.January Makamba (kushoto) akionyesha takwimu za upatikanaji wa umeme nchini katika Kipindi cha Mwaka Mmoja wa Mama kinachorushwa na Azam TV kuhusu mafanikio ya Sekta ya Nishati Katika Mwaka Mmoja wa Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita, Machi 24, 2022 mkoani Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Sita  imeundwa programu kubwa ya kuhakikisha kwamba  inapatikana nishati safi ya kupikia, salama na ya bei nafuu ambapo  propramu hiyo itazinduliwa wakati wa Bajeti ya Wizara ya Nishati ya mwaka 2022/2023.

Kuhusu upatikanaji wa mafuta vijijini, amesema yanafanyika mabadiliko ya kanuni ili kurahisisha ujenzi wa vituo vidogo vya mafuta vijijini ili hata kama mwananchi anataka lita moja ya mafuta awapo kijijini, awekewe mafuta yaliyo safi na ya bei nafuu.

Aidha alieleza kuwa, Wizara ya Nishati imeandaa programu kubwa ya kupeleka umeme vitongojini  na kazi kubwa inayofanyika sasa ni usimamizi makini wa miradi hii ya umeme vijijini inayoendelea ili ifanyike kwa ufanisi.

Katika mikakati ya kuleta unafuu wa bei ya gesi ya mitungi nchini, Waziri Makamaba alieleza kuwa, ndani ya mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Sita, Serikali imepata wawekezaji na eneo ili kuweza kushusha meli ya angalau tani Elfu 45 ambayo itasaidia gesi iingie kwa wingi na iwe nabei nafuu.

Baadhi ya Wahariri wa Vyombo vya Habari na wanazuoni wakiwa katika Kipindi cha Mwaka Mmoja wa Mama kinachorushwa na Azam TV ambapo Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba alikuwa akizungumza kuhusu mafanikio ya Sekta ya Nishati Katika Mwaka Mmoja wa Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita, Machi 24, 2022 mkoani Dar es Salaam.

Aliongeza kuwa, Mwezi wa Nne mwaka huu  atakaa na wauzaji wa gesi ili kuona namna ambavyo mfumo wa biashara unaweza kubadilishwa ili kurahisisha ufikaji wa gesi katika maeneo mengi nchini hivyo kuleta unafuu wa bidhaa hiyo.

Kuhusu usambazaji gesi, alisema kuwa, Katika mwaka ujao wa fedha imewekwa bajeti ya kujenga vituo mama na vituo dada kwa ajili ya kujaza  gesi ya kwenye magari na kushirikiana na pia kushirikiana na REA na TPDC  katika mradi wa kusambaza gesi majumbani katika njia ya bomba la gesi kutoka Dar es Salaam hadi Mtwara.

Vilevile, kuhusu uhifadhi wa mafuta, alisema kuwa kuna changamoto ya miundombinu ya kuhifadhi na kushusha mafuta ambayo imeanza kufanyiwa kazi  na Serikali imeanza mazungumzo na makampuni makubwa kuhakikisha kuwa inawekwa miundombinu bora ya kupakia mafuta, kuyahifadhi na kupakua tena ili kuyasafirsha nchi jirani.

Alizungumzia pia hifadhi ya mafuta ya kimkakati ambapo alieleza kuwa, zinaandaliwa kanuni mpya kwa ajili ya kuwa na hifadhi hiyo na kwamba Serikali inatambua kuwa sekta binafsi ina umuhimu katika kuhakikisha kuwa suala hilo linafanikiwa.

Kuhusu shughuli za udhibiti wa mkondo wa juu wa Petroli, Waziri wa Nishati alieleza kuwa, uongozi na utendji wa Tasisi inayosimamia mkondo huo  (PURA) imeimarishwa na katika kipindi cha mwaka mmoja yamefanyika maandalizi makubwa ya kwenda kwenye tenda  mwakani kwa ajili ya uwekezaji kwenye utafiti na kutafuta mafuta katika vitalu vilivyopo nchini ambapo mara ya mwisho Tanzania ilishiriki tenda hiyo mwaka 2013.

Alitanabaisha kwamba, PURA pia imeendelea kusimamia masuala mbalimbali katika Sekta ya Mafuta na Gesi kwa kwa umakini ikiwemo mikataba mbalimbali katika sekta ya gesi ili kuhakikisha kuwa gharama zinazosemwa na wawekezaji kuwa zimetumika katika uwekezaji huo nchini ni gharama halisi.

Kuhusu upatikanaji na usambazaji wa umeme nchini, alisema kuwa, mradi wa umeme wa  Julius Nyerere wa megawati 2115,  unaendelea kutekelezwa kwa mafanikio makubwa na kwa sasa mfumo wa usimamizi umebadilishwa kwani unasimamiwa kisayansi na Mhe. Rais, Samia Suluhu Hassan ameidhinisha fedha nyingi za kutekeleza mradi huo.

Alisema mradi huo una maeneo manne yanayoenda sambamba ambayo ni ujenzi wa bwawa,  ujenzi wa miundombinu ya kusafirisha umeme kutoka eneo la mradi hadi Chalinze mkoani Pwani, ujenzi wa kituo cha umeme Chalinze na  mradi wa matoleo kutoka chalinze-DSM- Tanga na Dodoma.   

Alieleza kuwa,  katika mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Sita, Serikali imesaini mikataba ya kutekeleza miradi ya usafirishaji umeme  kutoka eneo la mradi wa Julius Nyerere hadi Chalinze na kutoa umeme kutoka Chalinze kwenda maeneo mengine na sasa Serikali iko mbioni kusaini mkataba wa matoleo ya umeme kutoka kituo cha Chalinze.

Kuhusu upatikanaji wa umeme alisema kuwa, umeme unaopatikana ni megawati 1700 ambazo ni ndogo hivyo Serikali imeanzisha, kubuni na kuendeleza miradi mbalimbali ya uzalishaji umeme itakayofikisha megawati 5000 ifikapo mwaka  2025.

Kuhusu Jotoardhi alisema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita imeamua kushirikiana na washirika wa maendeleo ili kupata maeneo ya uhakika ya upatikanaji wa Jotoardhi na yakithibika kwamba yanaweza kuzalisha umeme nchi itaingia katika uzalishaji.

Aidha, kuhusu Nishati Jadidifu, alisema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita imekamilisha utayarishaji na uanzaji  wa utekelezaji wa takribani megawati 900 za umeme utakaotokana na upepo na jua ambazo zitaingizwa kwenye gridi ya Taifa.

Ad

Unaweza kuangalia pia

#LIVEDAY2: JUKWAA LA KODI NA UWEKEZAJI 2024

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.