
- Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekagua eneo la ujenzi wa hospitali ya Uhuru lenye ukubwa wa ekari 109 lililoko katika wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma. Akizungumza na wakazi wa kijiji cha Maduma wilayani humo, Waziri Mkuu amesema uamuzi wa Serikali ya kijiji hicho wa kutenga maeneo ya maendeleo ni wa kupigiwa mfano na vijiji vya maeneo mengine.

- “Uamuzi wenu wa kutenga maeneo ya miradi ya maendeleo umekuwa na tija, ndiyo maana Mheshimiwa Rais Magufuli aliposema ijengwe hospitali, hamkupata shida sababu eneo tayari lilikuwepo. Ninawapongeza wazee waliojitolea maeneo yao ili kuongeza kwenye eneo la hospitali,” amesema.
- Wazee waliotoa maeneo yao ni Mzee Meshack Njamasi (ekari 5.50), Mzee Jobu Malogo (ekari 3.50) na Bw. Nehemia Mwikwi (ekari 4.50). Ekari 95.5 zilizobakia, zimetolewa na Seriakli ya kijiji hicho.

- Waziri Mkuu aliwataka wakazi wa wilaya ya Chamwino wasibweteke bali wajipange na kila mmoja ajipange kufanya kazi kama ambavyo Rais Magufuli amekuwa akihimiza. “Ujenzi wa mji wa Serikali unaoendelea hivi sasa ni fursa kwenu. Na ujio wa hospitali hii ni fursa nyingine kwa wana-Chamwino hasa kwa vile ujenzi wake utatumia mfumo wa force account ambao unatoa fursa kwa wanajamii kushiriki kazi za miradi ya eneo husika,” amesema.

- Waziri Mkuu amesema ujenzi wa hospitali hiyo yenye hadhi ya wilaya ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) inayoelekeza wananchi wapatiwe huduma za matibabu huko huko waliko. “Hadi sasa tumeshajenga vituo vya afya 350 ili kusogeza huduma kwa wananchi na jumla ya hospitali za wilaya 67, zinajengwa nchi nzima kwa mwaka huu,” amesema.
- Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wakazi wa vijiji jirani, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Bw. Selemani Jafo amesema eneo la ujenzi wa hospitali hiyo liko umbali wa kilometa mbili kutoka barabara kuu ya Dar es Salaaam-Dodoma na kilometa tatu kutoka Ikulu ya Chamwino.
Ad