Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja na Naibu Katibu Mkuu, Kheri Abdul Mahimbali, tarehe 8 April, 2021, wameanza kazi rasmi katika Wizara ya Nishati baada ya kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, kushika nyadhifa hizo April 6, 2021.
Baada ya kuwasili katika Ofisi za Wizara ya Nishati, viongozi hao walifanya mazungumzo na Menejimenti ya Wizara pamoja na watumishi.
Akizungumza na Menejimenti ya Wizara pamoja na Watumishi, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja amewataka kufanya kazi kwa bidii, uaminifu na uadilifu.
Aidha, amewataka watumishi hao kufanya kazi kwa ushirikiano ili Wizara iweze kufanikisha shughuli zake zote, na malengo yaliyopangwa yaweze kutekelezeka kwa urahisi.
Vilevile, amewataka Wakuu wa Idara na Vitengo, kuwa wabunifu ili kuongeza ufanisi katika majukumu yao, na pia kuwawezesha watumishi waliopo chini yao ili wafanye majukumu yao kwa ufanisi.
Pia amewataka Wakuu hao wa Idara na Vitengo, kuweka usawa katika mgawanyo wa majukumu ili kila mtumishi aweze kuwatumikia watanzania kwa nafasi aliyonayo.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, wa Wizara ya Nishati, Kheri Abdul Mahimbali, amewataka watumishi wa Wizara kufanya kazi kwa ushirikiano na kuahidi kutumia uzoefu wake katika sekta ya Nishati ili kufanikisha majukumu ya Wizara.