- Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu amesema Serikali inaaangalia namna ya kufanya tathmini ya kupunguza bei ya kuunganisha umeme kwa wateja waliopo katika Miji na Manispaa ili huduma hiyo iweze kumfikia kila mmoja na kuondoa malalamiko.
- Mgalu alisema hayo, Desemba 6,2019, baada ya kubaini changamoto mbalimbali zilizoibuliwa na wawekezaji na wafanyabiara katika Mikutano ya Mashauriano baina ya Serikali,Wawekezaji na Wafanyabiashara, iliyofanyika katika Mikoa ya Morogoro, Pwani na Dar es Salaam.
- Alieleza kuwa changamoto kubwa iliyokuwa ikizungumzwa katika sekta ya nishati katika mikutano hiyo ni pamoja natofauti kubwa ya bei ya kuunganisha umeme kwa wateja waliopo katika Vijiji, Miji na Manispaa kuwa haziendani na mazingira halisi ya eneo husika.
- Mgalu alisema kuwa wafanyabiashara na wawekezaji wengi wamedai kuwa pamoja na serikali kuweka kiwango cha bei ya chini cha Shilingi 27,000 kwa kuunganishiwa umeme vijijini lakini wamekuwa wakitozwa kiwango kikubwa cha fedha tofauti na ilivyoelekezwa kwa madai kuwa wapo katika maeneo ambayo hayakupitiwa na mradi wa usambazaji umeme vijijini REA hali yakuwa wapo vijijini.
- Hata hivyo alisema kuwa serikali inatambua hali hiyo na kwamba inaangalia namna ya kupunguza bei ya kuunganisha umeme hadi maeneo hayo ya majiji na manispaa ili kila mwananchi apate huduma hiyo kwa urahisi na kwa bei nafuu.
- Pia, alibainisha endapo bei ya kuunganisha umeme katika Majiji na Manispaa kushuka, pia baada ya kukamilika kwa Mradi wa kufua umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rufiji wa Julias Nyerere utakaozalisha zaidi ya Megawati 2000 za umeme pia bei ya kununua umeme itashuka.
- Alitumia mkutano huo kuwaeleza wafanyabiashara na wawekezaji wenye changamoto za umeme katika maeneo yao kufika wizara ya nishati ili waweze kutatuliwa changamoto hizo kwa kuwa nishati ya umeme ni moyo wa uchumi na bila umeme hakuna viwanda.
- Mikutano hiyo ilihidhuriwa na Mawaziri, Naibu Mawaziri, Wakuu wa Taasisi na Mashirika ya Kiserikali na Binafsi ambapo tayari Mikoa saba imekwishafanya mikutano kama hiyo ambayo ni agizo la Rais Dkt, John Magufuli alilolitoa kwa Mawaziri baada ya kufanya kikao na wafanyabiashara hao mwanzoni mwa mwezi Juni mwaka huu, 2019.
Ad