WAZIRI KALEMANI AWASHA UMEME SAMUNGE NA DIGODIGO WILAYANI NGORONGORO

  • Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewasha umeme katika Vijiji vya Samunge na Digodigo vilivyopo wilayani Ngorongoro, mkoani Arusha na kumtaka Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa Umeme Vijijini wilayani humo kuongeza kasi zaidi.
K
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Samunge, wilayani Ngorongoro muda mfupi kabla ya kuwasha rasmi umeme kijijini hapo Mei 24, 2019. Kushoto ni Mzee Ambilikile Masapila, maarufu kama ‘Mzee wa Kikombe’ ambaye nyumba yake ni miongoni mwa zilizowashiwa umeme.
  • Akiwa katika ziara ya kazi hivi karibuni, kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme wilayani humo, Waziri Kalemani aliwasha umeme katika Taasisi kadhaa za Umma zikiwemo Shule, Vituo vya Afya na nyumba za wananchi, mojawapo ikiwa ya Mzee Ambilikile Masapila, maarufu kama Mzee wa Kikombe.
  • Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Samunge, muda mfupi kabla ya kuwasha rasmi umeme, Waziri Kalemani aliwaasa kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli kwa kuwajali na kuwapelekea maendeleo bila kubagua.
K
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Msingi Biskene iliyopo Kijijini Digodigo, Wilaya ya Ngorongoro alipofika kuwawashia rasmi umeme, Mei 24, mwaka huu akiwa katika ziara ya kazi.
  • “Leo tunawasha Samunge. Umeme huu umetoka umbali wa kilomita 35. Haikuwa kazi ndogo. Tumpongeze Rais wetu,” alisema Waziri.
  • Akifafanua zaidi, Dkt. Kalemani albainisha kuwa Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 24 kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme katika Mkoa wa Arusha.
  • Aidha, alitoa pongezi kwa kazi nzuri inayofanywa na wataalamu wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa Umeme Vijijini wilayani humo, Kampuni ya M/s Nipo Group Limited, ambayo ni kampuni ya wazawa.
K
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Serikali ngazi ya Mkoa, Wilaya na Kijiji, baada ya kumuwashia rasmi umeme Mzee Ambilikile Masapila maarufu kama Mzee wa Kikombe (wa tano kutoka kulia), nyumbani kwake Samunge, wilayani Ngorongoro, Mei 24 mwaka huu.
  • “Niwapongeze sana wataalamu. TANESCO mmefanya kazi nzuri sana hapa. Nawataka muongeze kasi zaidi. Isiishie hapa peke yake.”
  • Vilevile, Waziri alimpongeza Mzee Ambilikile kwa kuunga mkono juhudi za Serikali na kuunganishiwa umeme kwenye nyumba yake. Alitoa rai kwa watanzania wengine nchini kote, hususan wanaoishi vijijini, kuiga mfano wa Mzee huyo aliyewahi kupata umaarufu mkubwa miaka iliyopita, kulipia shilingi 27,000 tu ili waunganishiwe umeme kwenye makazi na biashara zao.
K
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati), akiteta jambo na Mzee Ambilikile Masapila maarufu kama ‘Mzee wa Kikombe’ nyumbani kwake, Samunge, Wilaya ya Ngorongoro, muda mfupi kabla ya kumuwashia rasmi umeme, Mei 24 mwaka huu.
  • Waziri pia, aliipongeza Benki ya NMB kwa kuifadhili kampuni ya Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa REA wilayani humo. Alizitaka Kampuni nyingine kuiga mfano huo kwa kutafuta Benki na Taasisi mbalimbali za Fedha ili ziwafadhili, waweze kutekeleza kazi zao kwa ufanisi zaidi.
  • “Kwangu ni tukio la kwanza, kushiriki pamoja na Benki ya kitanzania, ambayo imeonesha nia kufadhili Kmapuni za kitanzania ili nazo zipate fursa za kutekeleza miradi mbalimbali hapa nchini. Hongereni sana.”
  • Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza, ulizinduliwa wilayani mkoani Arusha, Agosti 19, 2017 na unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 24, ambapo ni Agosti, 2019. Na Veronica Simba – Arusha
Ad

Unaweza kuangalia pia

TANZANIA YAONGEZA HIFADHI SITA KWA KIPINDI CHA MIAKA MITATU

Na Pamela Mollel,Ngorongoro Tanzania imeongeza hifadhi sita (6) kwa kipindi cha miaka mitatu kutoka hifadhi …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *