TUNATAKA KURAHISISHA MAZINGIRA BIASHARA YA MADINI – BITEKO

  • Waziri wa Madini Doto Biteko amesema Serikali kupitia Wizara yake inalenga kurahisisha Mazingira ya Biashara ya Madini ikiwemo kuwalea wachimbaji na kuwataka wafanyabiashara na wachimbaji kuhakikisha wanajisimamia wenyewe kwa manufaa yao na Taifa.
  • Waziri Biteko ameyasema hayo alipokutana na viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA), wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho Sam Mollel ofisini kwake jijini Dodoma Aprili 10, kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayohusu biashara ya madini nchini.
WATENDAJI
Baadhi ya Watendaji kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini wakifuatilia kikao baina ya Waziri wa Madini na Ujumbe wa Chama Cha Wafanyabiashara ya Madini Tanzania (TAMIDA).
  • Amekitaka chama hicho kuendelea kushirikiana na wizara kwa lengo la kusukuma mbele Sekta ya Madini ikiwemo kuhakikisha biashara ya madini inafanyika katika mazingira yenye kuzinufaisha pande zote na kuwasisitiza viongozi hao kuhakikisha wanachama wao wanafuata taratibu wanapofanya biashara ya madini.
  • Awali, kabla ya kujibu hoja zilizowasilishwa na chama hicho, Waziri Biteko amekipongeza  chama  hicho kwa kuwa kimekuwa kikitoa njia mbadala pindi kinapowasilisha changamoto na kero  zake badala ya kuishia kulalamika na kuongeza, “wizara inaona fahari kwa hilo na tunayachukulia kwa umuhimu maoni yenu,”.
WAZIRI WA MADINI
Baadhi ya Viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara ya Madini Tanzania (Tamida) wakifuatilia mkutano wao baina ya Waziri wa Madini Doto Biteko , Naibu Waziri na Viongozi wa Wizara.
  • Akizungumzia suala la kodi ya ongezeko la thamani na kodi ya zuio ambayo imeondolewa kwenye uchimbaji mdogo, Waziri Biteko amekitaka Chama hicho kutoa nafasi kwa serikali kufuatilia suala hilo. Waziri Biteko ameleeza hilo kufuatia hoja iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameeleza kuwa, katika mkoa wa Arusha, kodi hiyo bado inatozwa licha ya serikali kuiondoa.
  • Aidha, Waziri Biteko ametolea ufafanuzi wa changamoto kadhaa zilizowasilishwa na Mwenyekiti Sam Mollel kwa niaba ya chama hicho ikiwemo. Kuhusu bei elekezi, Waziri Biteko  amesema wizara itaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha suala hilo linakuwa shirikishi.
  • Waziri Biteko amesema hilo baada ya TAMIDA kutoa pongezi kwa serikali kwa kutoa nafasi kwa wadau kukaa pamoja na serikali kujadili suala la bei elekezi ambapo Mwenyekiti huyo amemweleza Waziri Biteko kuwa, katika hilo, serikali na wadau wameanza vizuri.
TEKO-3
Waziri wa Madini Doto Biteko (wa kwanza kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina yake na Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA). Wengine wanaofuatilia ni Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa (kulia kwa Waziri) na Ujumbe wa Chama hicho.
  • Akitolea ufafanuzi kuhusu suala la kurejesha maonesho ya madini jijini Arusha, Waziri Biteko amesema suala la maonesho ya madini kufanyika arusha inawezekana lakini si kwa madini ya Tanzanite, na kuongeza kuwa, serikali imedhamiria kufanya shughuli zote zinazohusu madini hayo ndani ya ukuta unaozunguka machimbo ya mirerani lakini pia ikilenga kuubadilisha  mji wa  mirerani ufanane na madini hayo.
  • Aidha, Waziri Biteko amezungumzia suala la kuongeza wataalam wa kuthamini madini ya Tanzanite Mirerani na kueleza kuwa, kutokana na unyeti na umuhimu wa suala hilo, tayari serikali imeanza kulifanyia kazi ili kuhakikisha inaongeza idadi ya wataalam kuwezesha shughuli za uthamini Mirerani, kufanyika kwa wakati. Ufafanuzi huo umetolewa baada ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel kuwasilisha changamoto ya kuwepo na  upungufu wa wataalam hao.
WAZIRI
Waziri wa Madini Doto Biteko na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo wakimsikiliza Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel wakati akizungumza jambo katika kikao hicho. Wengine wanaofuatilia ni Kamishna wa Madini David Mulabwa na mmoja wa wajumbe wa chama hicho, Abe Latif.
  • Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akizungumza katika kikao hicho, ametaka kuanzishwa haraka kwa soko la Madini jijini Arusha na kueleza kuwa, kwa upande wa wizara itahakikisha inashirikiana na serikali ya mkoa kuhakikisha soko hilo linaanzishwa haraka. Naibu Waziri Nyongo amesema hayo akijibu hoja ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameleeza katika kikao hicho kuwa, Chama hicho kinaunga mkono Serikali kuhusu uanzishwaji wa masoko ya madini na kuitaka serikali ione umuhimu wa kuanzisha soko La madini la madini mkoani arusha kuwezesha biashara ya madini ya vito kufanyika kwa urahisi.
  • Kuhusu vibali vya Wataalam wa masuala ya ukataji na unga’rishaji wa madini kutoka nje ya nchi, Naibu Waziri Nyongo amesema kuwa, ni kweli kwamba serikali inawahitaji wataalam hao kwa kuwa pia watawezesha kutoa ujuzi huo kwa wataalam wa ndani ili kuhamasisha viwanda vya ukataji madini na kuongeza, “ serikali inaangalia namna ya kulipatia ufumbuzi suala hilo kwa kushirikiana na mamlaka zinazohusika kwa sababu pia tunataka watu wetu wanufaike na utaalam huo”,.
  • Pia, ameongeza kuwa, kutokana na kulichukulia suala la uongezaji thamani madini kwa umuhimu, inakitegemea kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kwa ajili ya kuzalisha wataalam na kukitaka chama hicho kusaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa katika kituo hicho kwa kuwa hivi sasa idadi bado ni ndogo.
  • Kikao hicho cha Waziri na TAMIDA ni cha kwanza tangu kuteuliwa kwa Waziri wa Madini Doto Biteko kuiongoza wizara husika.
Ad

Unaweza kuangalia pia

SOKO LA MDINI ULANGA LA KUSANYA MILIONI 396 NDANI YA MIEZI 5

Waziri wa Madini Doto Biteko amesema tangu kuanzishwa kwa soko la madini Ulanga wamenunua madini …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *