RC WANGABO AINGILIA KATI UJENZI WA STENDI KUU YA MABASI SUMBAWANGA BAADA YA KUONA UNASUASUA

Mkuu wa mkoa wa Rukwa mh. Joachim Wangabo (katikati) alipotembelea Stendi kuu ya Mabasi Sumbawanga ili kujionea maendeleo ya ujenzi wa stendi,Kulia ni mkurugenzi wa Sumry Enterprises Ltd Humud Sumry pamoja na Meneja TARURA Manispaa ya Sumbawanga Mhandisi Suleiman Mziray

Baada ya kuona ujenzi wa Stendi Kuu ya Mabasi Sumbawanga unasuasua Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ametembelea Stendi hiyo iliyotarajiwa kumalizika mwezi Juni Mwaka huu ili kujionea hatua iliyofikiwa na kutaka kupewa maelezo juu ya mkwamo wa ujenzi huo ambao ni miongoni mwa miradi ya kimkakati ya mkoa katika kuongeza mapato ya Manispaa ya Sumbawanga.

Mh. Wangabo amesema kuwa ukamilifu wa stendi hiyo utaongeza shughuli nyingi za kiuchumi kwa wananchi hasa wajasiliamali pamoja na wafanyabiashara mbalimbali wa ndani na nje ya mkoa kutokana na miundombinu iliyomo kwenye stendi hiyo inayotarajiwa kuongeza ubora wa utoaji wa huduma kwa abiria zaidi ya 400 kwa wakati mmoja.

Ad
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kushoto) akiendelea na ukaguzi wa vyumba vya kukatia tiketi pamoja na kituo kidogo cha polisi katika jengo la abiria Stendi kuu ya mabasi Sumbawanga.

“Kilichobakia ili hii stendi kuu yam abasi ifanye kazi ni kitu kidogo, ni asilima nane tu na hiyo 8% ni vitu vidogo vidogo ambavyo tunaweza kuvifanyia kazi, mkurugenzi ningependa kuona stendi hii kuu ya mabasi inafanya kazi mwanzoni mwa mwezi Oktoba, jitahidini sana kutatua changamoto ya fedha ambayo amesema hapa mkandarasi mumlipe, ‘ame-raise certificate’ ya shilingi milioni 350 mlipeni,”

“Stendi ikianza kufanya kazi mtaendelea kuingiza mapato mtalipana tena polepole wakati mnafuatilia hela hazina na mahala pengine kama mlivyosema kuliko kukaa kimya kunakuwa na mdororo, halafu kunakuwa na maswali mengi yasiyokuwa na majibu lakini pia tunapokaa muda mrefu kuna vinaweza kuanza kupotea halafu maumivu ya stendi kutofanya kazi yakawa makubwa Zaidi,” Alisema.

Aidha, Amemuagiza mkurugenzi kuhakikisha anakamilisha miundombinu ya maji kabla ya stendi hiyo kuanza kutumiaka Pamoja na kumtaka kuwa makini na watumiaji wa huduma zinazopatikana katika stendi hiyo ikiwemo utunzaji wa vyoo na kumtaka Katibu Tawala wa Mkoa kuhakikisha Mkandarasi analipwa fedha anazodai ili stendi hiyo ikamilike kwa wakati.

Stendi kuu ya mabasi Sumbawanga sehemu ya kupaki magari

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga James mtalitinya alikitri kuwa fedha zilizotengwa kwaajili ya ujenzi wa Stendi huo tayari zimekwisha na chanzo pekee cha fedha kilichobaki kwaajili ya kumlipa mkandarasi ni makusanyo ya ndani ya halmashauri Pamoja na kutegemea kuomba fedha kutoka serikali kuu.

“Tumekuwa tukishauriana na mkandarasi hasa aweze kukamilisha jengo hili la abiria angalau aweze kufunika hizo ‘fisher board’ angalau muonekano wa jengo na huduma zinazoweza kuanza ziweze kuanza kwasababu mahitaji makubwa hap ani maji Pamoja na ukamilishaji wa muonekano wa jengo, kwahiyo hayo tumeendela kushauriana nae ili kuyakamilisha na stendi ianze, ndio maana kazi nyingine zote tumezisimamisha kwa sasa hivi,” Alisema.

Wakati akisema taarifa ya ujenzi wa stendi hiyo Meneja wa Wakala wa Barabara za Mjini na Vijiji (TARURA) Manispaa ya Sumbawanga Mhandisi Suleiman Mziray alisema kuwa katika mkataba wa awali stendi hiyo ilitakiwa kujengwa pamoja na jengo la chini pekee kwa gharama ya shilingi bilioni 5.4 lakini kamati ya uchumi na fedha ya Manispaa ilishauri lijengqe ghorofa na hivyo gharama kuongezeka na kufikia shilingi Bilioni 5.9.

“Vilevile wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwa na kazi zinaonekana zinaongezeka ambapo ikapelekea mpaka mkataba tulionao sasa hivi kufikia bilioni 7.2 na kazi mheshimiwa Mkuu wa Mkoa ilianza tarehe 24, Aprili 2019 na inatemewa kumalizika tarehe 20, Septemba 2020, na kwa ujumla ujenzi umekamilika kwa asilimia 92,” Alisema.

Aidha, Mkurugenzi wa Kampuni ya Sumry Enterprises Humud Sumry alisema kuwa jambo kubwa linalokwamisha ujenzi wa stendi hiyo ni upatikanaji wa fedha ambapo wanadai karibu shilingi bilioni 2 huku akionyesha wasiwasi wa kulipwa fedha hizo kwa wakati na kutoa maombi yake, “ Maombi yangu, serikali iangalie kuisaidia manispaa ili kuonekana wapi pesa inapatikana ili kumalizia kilichobaki na stendi itumike na kuleta tija kama mradi ulivyokususdiwa.”

Stendi hiyo ya Mabasi ikianza kutumika itakuwa na Jengo la abiria 400, kituo cha polisi, Baa, Vymbwa 16 vya kulala wageni, Sehemu ya Mazoezi (GYM), ofisi 24 za kukatia tiketi, vyoo vya kulipia, vyumba vya benki na ATM, vibanda vya mlinzi na maduka 100.

Ad

Unaweza kuangalia pia

Uzinduzi wa Jengo Jipya la Makao Makuu ya UCSAF Dodoma: Kuimarisha Mawasiliano Vijijini

25 Aprili 2024, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *