UJENZI WA BOMBA LA MAFUTA KUZALISHA AJIRA 10,000

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimlaki mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni alipowasili kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Rais wa Jamhuri ya Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni tarehe 13 Septemba, 2020 amefanya ziara ya kikazi ya siku 1 hapa nchini ambapo ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kushuhudia utiaji saini wa makubaliano ya kukamilisha majadiliano ya utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta la kutoka Hoima nchini Uganda hadi bandari ya Tanga nchini Tanzania. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimlaki mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni alipowasili kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Utiaji saini huo umefanyika katika uwanja wa ndege wa Chato Mkoani Geita ambapo Waheshimiwa Marais hao pia wametia saini waraka wa pamoja wa kuagiza kuanza haraka kwa utekelezaji wa mradi huo.

Ad

Hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Tanzania na Uganda wakiwemo Mawaziri, Wanasheria Wakuu wa Serikali, Wakuu wa Mikoa, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, viongozi na wataalamu wa taasisi mbalimbali za Serikali na viongozi wa vyama vya siasa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakitia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Waziri wa Nishati wa Tanzania, Dkt. Medard Kalemani amesema bomba litakalojengwa litakuwa na urefu wa kilometa 1,445 ambapo kilometa 1,149 kati yake zinapita nchini Tanzania, litapita katika mikoa 8, wilaya 24 na vijiji 280 hapa nchini, litakuwa na uwezo wa kupitisha mapipa 216,000 kwa siku, litazalisha ajira 10,000 na kwamba kwa miaka 25 ya mradi huo Tanzania itapata mapato ya kiasi cha shilingi Trilioni 7.5.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania Prof. Adelardus Kilangi amesoma maelekezo ya pamoja yaliyotolewa na kutiwa saini na Waheshimiwa Marais ambapo wameelekeza kuwa kila nchi ichukue hatua za haraka ili kutia saini mkataba kati ya nchi husika na kampuni zinazotekeleza mradi huo, kila nchi ianze kwa haraka mashauriano ili kusaini mikataba midogo inayohusika katika mradi huo na pia kila nchi ichukue hatua ili kuwezesha utekelezaji wa haraka wa mradi huo. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakishuhudia mawaziri wa Nishati wa nchi zao ( Mhe. Mary Goretti Kitutu wa Uganda na Dkt. Medard Kalemani wa Tanzania) wakitia saini mkataba wa kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Katika hotuba yake, Mhe. Rais Magufuli amempongeza na kumshukuru Mhe. Rais Museveni kwa kuchukua hatua madhubuti za kutafuta mafuta nchini mwake, kukubali bomba lipitishwe nchini Tanzania na pia kuridhia asilimia 60 ya faida ichukuliwe na Tanzania (ambako bomba linapita kwa Zaidi ya asilimia 70) ilihali Uganda ikichukua faida kwa asilimia 40.

Mhe. Rais Magufuli amesema kutekelezwa kwa mradi huo ni ushindi mkubwa wa kiuchumi kwa Uganda na Tanzania pamoja na ukanda wote wa Afrika Mashariki na ameahidi kuwa Tanzania itasimamia masuala yote yaliyobaki ili utekelezaji uanze haraka kwa manufaa ya Watanzania na Waganda.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongea mbele ya mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Aidha, Rais Magufuli ameeleza kuwa kutekelezwa kwa mradi huo kutarahisisha upelekaji wa gesi ya Tanzania nchini Uganda kupitia njia hiyo hiyo na pia kutarahisisha usafirishaji wa mafuta yanayotafutwa katika mbuga ya Wembele nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Rais Museveni ameelezea kufurahishwa kwake na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa mradi huo na amebainisha kuwa kwa sasa jambo muhimu ni kuanza utekelezaji wa mradi ili wananchi waanze kuona manufaa yake badala ya kupoteza muda mwingi zaidi katika majadiliano.

Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni akiongea baada ya kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Rais Museveni amesema utafiti uliofanywa katika asilimia 40 ya bonde la mto Albert huko Hoima nchini Uganda umebaini kuwepo kwa mapipa bilioni 6.5 ya mafuta ghafi na kwamba zipo dalili njema kuwa asilimia 60 za eneo ambalo halijatafitiwa pia kuna mafuta na kwamba Uganda inatarajia kupata mafuta mengine katika ukanda wa Kadamu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimshukuru kwa hotuba nzuri Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Amesimulia kuwa baada ya kubaini kuwa wataalamu wa mataifa ya nje walikuwa wakimyumbisha katika mpango wake wa kupata mafuta nchini Uganda, aliamua kuchukua hatua za kuwasomesha vijana wa Uganda na baadaye vijana hao wakafanya utafiti na kisha kupata mafuta ambayo leo yamefikia hatua ya kuchimbwa, na pia ametoa wito kwa wananchi wa Tanzania na Uganda kuamka na kuchapa kazi za uzalishaji mali kwa maendeleo badala ya kuishia kuzalisha kwa kujikimu.

Rais Museveni amerejea nchini Uganda.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni akimsindikiza mgeni wake anayeagana na mawaziri wa Tanzania wakati akiondoka kurejea nyumbani baada ya kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama wakipunga mikono kumuaga Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakati akiondoka kurejea nyumbani baada ya kutia saini Waraka wa Pamoja Unaoagiza kuanza haraka mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) kwenye sherehe fupi iliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Chato mkoani Geita Jumapili Septemba 13, 2020

Ad

Unaweza kuangalia pia

BANDARI YA DAR ES SALAAM INAPANUKA NA KUIMARIKA: HATUA MUHIMU KWA UCHUMI WA TANZANIA

Bandari ya Dar es Salaam ni kitovu muhimu cha biashara na uchumi wa Tanzania, na …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *