Wizara ya Kilimo imetoa wito kwa wawekezaji wa ndani ya nchi kushirikiana na Wakala wa Mbegu (ASA) kuzalisha mbegu bora nyingi na zenye tija na kuwezesha wakulima kupata kwa gharama nafuu.
Wito huo umetolewa jana (19.10.2020) na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya alipotembelea na kukagua utendaji kazi wa shamba la Mbegu la ASA Mbozi mkoani Songwe.
“Nakaribisha wawekezaji katiuka uzalishaji mbegu lakini lengo la wizara ni kupata mbegu bora ambazo zitamfikia mkulima kwa gharama nafuu na kwa wakati “alisema Kusaya.
Kusaya ambaye aliambatana kwenye ziara hiyo pamoja na makampuni yanayojihusisha na uzalishaji mbegu pamoja na ASA ikiwemo Jeshi la Kujenga Taifa aliwataka kuendelea kutumia ardhi kubwa iliyopo kuzalisha mbegu bora zinazohitajika na wakulima wa Tanzania na kupunguza utegemezi wa nje.
“Natoa rai kwa Jeshi la KLujenga Taifa njooni hapa Mbozi mshirikiane na wakala wetu ASA mzalishe mbegu bora ili ushirikano wetu usaidie Taifa kuwa na mbegu bora zilizotafitiwa na watanzania wenyewe badala ya mbegu za kutoka nje ya nchi” alisisitiza Kusaya.
Akitoa taarifa ya hali ya upatikanaji mbegu za mazao nchini, Mtendaji Mkuu wa ASA Dkt. Sophia Kashenge alisema wakala huo unayo mashamba 10 yanayozalisha mbegu takribani asilimia 21 hdi 25 inayotumika nchini.
Dkt. Sophia aliongeza kusema katika mwaka 2020/21 wakala kwa ushirikiano na makampuni binafsi na taasisi za umma umeweza kuzalisha mbegu mbalimbali za mazao tani 5,600
Kuhusu uzalishaji wa mbegu bora za michikichi aina ya Tenera zenye kutoa mavuno mengi,Dkt. Sophia alisema ASA tayari imefanikiwa kuzalisha miche 342,000 katikam vituo vyake vitatu ambayo itagawiwa kwa wakulima wa Kigoma,Morogoro na Mbozi.Katibu Mkuu Kilimo alipongeza ASA kwa kuzalisha miche bora ya michikichi 42,000 katika shamba lake la Mbozi hali itakayosaidia kuongeza wigo wa uzalishaji michikichi kama livyoagizwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Kusaya alisema Tanzania kwa sasa inatumia zaidi ya Shilingi Bilioni 443 kwa ajili ya kuagiza mafuta ya kula nje ya nchi hivyo lengo la seriklai kuhamasisha kilimo cha michikichi ili nchi ijitosheleze kwa mafuta.Katika hatua nyingine Katibu Mkuu huyo alitembelea Kituo cha Utafiti wa kahawa (TACRI) Mbimba wilayani Mbozi na kufahamishwa kuwa kituo hicho kimefanikiwa kuzalisha na kusambaza miche bora ya kahawa milioni 11.2 kwa wakulima wa mikoa ya Songwe, Mbeya,Rukwa na Katavi katika kipindi cha mwaka 2008 hadi 2020.
Akitoa taarifa ya kituo hicho Meneja wa TACRI Mbimba Isaack Mushi aliongeza kusema kituo kimefanikiwa pia kuwafikia wakulima 74,565 katika wilaya 10 za Nyanda za Juu Kusini na kuwapa elimu ya kilimo bora cha kahawa.“Msimu wa 2020/21 tunatarajia kuzalisha na kusambaza miche bora ya kahawa milioni 4.5 kwa wakulima hali itakayokuza uzalishaji kahawa” alisema Mushi.
Kuhusu takwimu za unywaji kahawa Mushi alisema watanzania wanakunywa kahawa asilimia 7 tu ya kahawa yote inayozalishwa nchini hali inayopunguza upatikanaji wa soko.