MKURABITA INATEKELEZA KWA VITENDO DIRA YA MAENDELEO YA TAIFA 2025

Katika  kipindi cha miaka minne (2005 – 2008) uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika na Pato la Taifa lilikua kwa wastani wa asilimia 7.2 kwa mwaka kuongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi katika sekta za viwanda, ujenzi na fedha.

Pamoja na mwaka 2009 kuwa ni mwaka ambao kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa inatarajiwa kupungua kutokana na athari za msukosuko wa uchumi wa dunia, takwimu za Pato la Taifa kwa robo mwaka zinaonesha kuwa, katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka (Januari – Machi 2009) uchumi wa Taifa ulikua kwa asilimia 5.6 ikilinganishwa na asilimia 6.2 katika kipindi kama hicho mwaka 2008.

Ad

Ingawa uchumi wa Tanzania umekuwa ukikua katika siku za hivi karibuni matokeo ya ukuaji huo wakati mwingine hayawafikii watu masikini katika jamii ikiwa na ina maana kuwa kasi ya upunguzaji umasikini bado hairidhishi.

Serikali imeanzisha sera na programu kadhaa zenye lengo la kukuza uchumi na kupunguza umasikini kwa kupanua ushiriki wa Watanzania wote katika shughuli za kiuchumi.

Sera ya Uwezeshaji Kiuchumi ndiyo msingi wa juhudi hizo za Serikali, ikiwa na malengo ya kuwawezesha Watanzania kumiliki, kuendesha na kunufaika na uchumi wao wenyewe ikiwa ni pamoja na kuondoa baadhi ya vikwazo vinavyowakabili Watanzania katika shughuli za kiuchumi.

Moja ya mawazo ambayo Serikali iliyazingatia kama mbinu rahisi ya kupanua ushiriki wa Watanzania katika uchumi ni pamoja na kuwaingiza watu wengi zaidi katika uchumi rasmi na wenye kutumia kumbukumbu.

Miongoni mwa programu hizo ni pamoja na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania (MKURABITA) ulioanzishwa na Serikali kwa lengo la kuhakikisha kuwa biashara na rasilimali za wanyonge zilizo kwenye sekta isiyo rasmi zinarasimishwa kuziwezesha kutambulika kisheria.

Akiwasilisha Hotuba ya Makadirio ya Bajeti ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2018/19, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Mkuchika anasema Serikali imeendelea kutekeleza jukumu la kuandaa na kusimamia mfumo wa Kitaifa wa umiliki wa rasilimali na uendeshaji wa biashara nchini unaotambulika na kukubalika kisheria.

Anaongeza kuwa katika kipindi cha mwaka 2017/18, MKURABITA imefanikiwa kuwajengea uwezo Wakulima 589 na viongozi 89 jinsi ya kutumia hati za haki Miliki za Kimila kupata Mitaji katika Benki na Taasisi zingine za Fedha katika Halmashauri za Wilaya za Misungwi, Mpwapwa na Serengeti.

Waziri Mkuchika anasema MKURABITA kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Urambo imefanikisha kuanzishwa kwa Kituo Kimoja cha Urasimishaji wa Biashara, ambapo huduma muhimu  ikiwemo utoaji wa namba ya utambulisho wa mlipa kodi (TIN), usajili wa jina la biashara (BRELA) na utoaji leseni za biashara zinapatikana sehemu moja.

“Hadi kufikia Machi, 2018 Kituo kimesajili biashara 380 ambapo Shilingi milioni 4.5 zimekusanywa kutokana na ada za leseni na wafanyabiashara 79 wamepata leseni na 200 wamefungua akaunti katika benki kwa ajili ya kuweka akiba na kukopa fedha” anasema Waziri Mkuchika.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuchika anasema MKURABITA pia imefanikisha kutoa mafunzo ya urasimishaji na uendeshaji wa biashara kwa Wafanyabiashara 100 katika Wilaya za Kusini Unguja (50) na Micheweni, Pemba (50) ambapo wafanyabiashara 10 wamesajili Majina ya Biashara na kupata Leseni za kuendesha Biashara.

Akifafanua zaidi Mkuchika anasema MKURABITA pia iliwezesha Wafanyabiashara 13 waliorasimisha biashara zao Unguja na Pemba kushiriki kwenye Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yaliyofanyika Nchini Burundi mwezi Desemba, 2017.

Mkuchika anasema MKURABITA Kwa kushirikiana na Ofisi za Taifa za Takwimu Tanzania Bara na Zanzibar, imeanza kufanya utafiti kuhusu Sekta isiyo Rasmi nchini kwa lengo la kubaini ukubwa na thamani ya Sekta isiyo, ambapo utafiti wa Majaribio umefanyika katika Mikoa sita (6) ya Tanzania Bara na miwili (2) Zanzibar.

Anaitaja Mikoa hiyo kuwa ni Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Mtwara, Mwanza, Tanga, Mjini Magharibi na Kusini Pemba na utafiti huo ulilenga kuona kama methodolojia, sampuli na madodoso yaliyoandaliwa yanaweza kuleta matokeo tarajiwa juu ya ukubwa wa Sekta isiyo Rasmi kwa sasa.(Na Ismail Ngayonga)

Ad

Unaweza kuangalia pia

BANDARI YA DAR ES SALAAM INAPANUKA NA KUIMARIKA: HATUA MUHIMU KWA UCHUMI WA TANZANIA

Bandari ya Dar es Salaam ni kitovu muhimu cha biashara na uchumi wa Tanzania, na …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *