- Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani amekutana na Balozi wa Angola nchini Tanzania, Sandro De Oliveira na kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano katika utafiti wa Mafuta na Gesi pamoja na ununuzi wa mafuta.
- Mazungumzo kuhusu ushirikiano huo yalifanyika tarehe 14/11/2019 jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Kaimu Kamishna wa Petroli na Gesi, Marwa Petro, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Dkt. James Mataragio na Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Ubalozi wa Angola nchini.
- Waziri wa Nishati, alisema kuwa Tanzania ipo tayari kushirikiana na nchi hiyo ya Angola kwa kuwa tayari inauzoefu kwenye masuala ya utafiti wa mafuta na gesi na tayari imeshagundua mafuta.
- Aliongeza kuwa Tanzania ina maeneo kadhaa yenye viashiria vya mafuta mfano Bonde la Eyasi Wembere na Ziwa Tanganyika hivyo Serikali inafanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha kuwa nchi inapata mafuta kama ilivyo kwa nchi hiyo ya Angola ambayo ipo pia katika Umoja wa Nchi zinazozalisha Mafuta duniani (OPEC).
- Aidha alitoa muongozo wa nini kinachotakiwa kufanywa baada ya mazungumzo ya viongozi hao wawili ili lengo hilo la mashirikiano liweze kufanyiwa kazi na wataalam wa nchi hizo mbili likiwemo suala la nchi ya Angola kuiuzia mafuta Tanzania.
- Kwa upande wake, Balozi Oliveira alisema kuwa Wakuu wa nchi za Angola na Tanzania wanafahamu kuhusu suala hilo hivyo ni muhimu kwa watendaji wa pande zote mbili kulifanyia kazi suala hilo na kutoa taarifa kwa viongozi hao Wakuu badala ya kusubiri viongozi hao kuulizia utekelezaji wa suala hilo.
- Wakati huohuo, Waziri wa Nishati alikutana na watendaji wa kampuni ya ORMAT ya nchini Marekani ambao wameeleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi Tanzania (TGDC) katika masuala ya utafiti na uzalishaji umeme kwa kutumia Jotoardhi.
- Meneja Mwandamizi wa Maendeleo ya Biashara wa kampuni hiyo, Raphael Swerdlow alimueleza Waziri wa Nishati kuwa kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 1965 inazalisha umeme kutokana Jotoardhi kwenye maeneo mbalimbali duniani ikiwemo nchini Kenya ambapo wanazalisha megawati 139.
- Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani aliwaeleza watendaji wa kampuni hiyo kuwa, Serikali inahitaji kampuni makini na yenye nia ya dhati ya kushirikiana na TGDC ili kuweza kuzalisha umeme kutokana na chanzo hicho ambacho bado hakijaanza kuzalisha umeme nchini licha ya kuwa na maeneo mengi nchini yenye viashiria vya Jotoardhi.
Ad