RAIS MAGUFULI ATUNUKIWA SHAHADA YA HESHIMA YA UDAKTARI WA FALSAFA YA UDOM

  • Rais Dkt. John Pombe Magufuli  ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa katika Sayansi (Doctor of Science Honoris Causa) ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
  • Rais Magufuli aliyeongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli ametunukiwa shahada hiyo na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma Mhe. Benjamin William Mkapa (Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu) katika sherehe za mahafali ya 10 ya chuo hicho zilizofanyika katika ukumbi wa Chimwaga Jijini Dodoma.
33-01
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akipokea cheti kutoka kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa mara baada ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu (PhD) katika Sayansia wakati wa Mahafali ya 10 ya chuo hicho leo tarehe 21/11/2019 jijini Dodoma. Rais Magufuli ametunukiwa PhD hiyo ikiwa ni kutambua mchango wake katika maendeleo ya nchi ambapo anakuwa mtu wa tatu kutunukiwa Shahada hiyo na UDOM akitanguliwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete na Mzee Rashid Mfaume Kawawa.

 

  • Sherehe hizo zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa aliyeongozana na Mkewe Mama Mary Majaliwa, Mawaziri, Wabunge, Mabalozi wa nchi mbalimbali, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Mikoa, viongozi wa Dini, viongozi wa siasa na wasomi.
  • Wasifu wa Dkt. John Pombe Magufuli uliosomwa na Prof. Davis George Mwamfupe umeeleza kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kimeamua kumtunuku Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa Mhe. Rais Magufuli kwa kutambua mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Tanzania kwa kipindi kifupi cha miaka 4 ya uongozi wake kwenye sekta za elimu, nishati, miundombinu, uchukuzi, maji, mawasiliano, maliasili, utalii, afya, madini na kilimo.
55-01
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa (kulia) akimpongeza Rais Dkt. John Pombe Magufuli mara baada ya kumtunuku Shahada ya Heshima ya Uzamivu (PhD) katika Sayansi, wakati wa Mahafali ya 10 ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) leo tarehe 21/11/2019 jijini Dodoma. Katikati ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof.Josephat Bee.
  • UDOM imeeleza kuwa kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya 2025 inayoelekeza Tanzania kuingia katika uchumi wa kati imefanywa kwa mafanikio makubwa na imetaja baadhi ya maeneo ya mafanikio kuwa ni utoaji wa elimu bila malipo kwa shule za msingi na sekondari, kujenga miundombinu na kuongeza mikopo ya wanafunzi wa vyuo vikuu, kuongeza uzalishaji wa nishati ya umeme na kuanza ujenzi wa Bwawa la Nyerere, kujenga barabara, reli ya kisasa (SGR), bandari na viwanja vya ndege.
  • Maeneo mengine ni kuongeza upatikanaji wa maji ambapo hadi Februari 2019 miradi 65 ya maji iliyowanufaisha Watanzania Milioni 25.36 imetekelezwa, kuunganisha Zanzibar na mkongo wa Taifa na kuweka mfumo wa kusimamia mawasiliano (TTMS), kununua ndege 11 kwa ajili ya kuimarisha usafiri wa anga na kukuza utalii, kudhibiti ujangili, kuboresha sekta ya afya (kwa kujenga hospitali 69, vituo vya 352, kuongeza bajeti ya dawa kutoka Shilingi Bilioni 31 hadi Bilioni 270 na kununua vifaa tiba), kusimama na kuongeza mapato ya madini na kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula hali iliyoweza kuwepo chakula cha kutosha na cha ziada.
22-01
Rais Dkt. John Pombe Magufuli (kulia) akifurahia jambo na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mhe.Benjamin Mkapa mara baada ya kutunukiwa Katika mahafali ya hayo Rais Dkt. John Pombe Magufuli ametunukiwa Shahada ya heshima ya Udaktari wa Falsafa (Phd) katika Sayansi ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuleta maendeleo ya nchi.katika Sayansia wakati wa Mahafali ya 10 ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) leo tarehe 21/11/2019 jijini Dodoma. Rais Magufuli ametunukiwa PhD hiyo ikiwa ni kutambua mchango wake katika maendeleo ya taifa ambapo anakuwa mtu wa tatu kutunukiwa digrii hiyo na chuo hicho akitanguliwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete na Mzee Rashid Mfaume Kawawa
  • Akizungumza baada ya kutunukiwa shahada hiyo, Rais Magufuli amekishukuru Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kumtunuku shahada hiyo na amebainisha kuwa awali haikuwa rahisi kwake kukubali kutunukiwa shahada ya Udaktari wa Falsafa pasipo kuisomea darasani, lakini baadaye alikubali kwa kuwa anaamini shahada hiyo imetolewa kwa kutambua kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wake.
  • “Kutokana na maisha niliyokulia sikuwahi kuzoea vitu vya burebure (dezo), na hapa dunia nimejifunza kuwa hakuna kitu cha bure, hata hivyo nimetambua kuwa shahada hii imetolewa kwa kutambua mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa miaka 4, hivyo hii ni heshima kwa Watanzania wote, wafanyakazi, wakulima, wafugaji na wavuvi hasa wanaolipa kodi” amesema Mhe. Rais Magufuli.
11-01
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akifurahia jambo na Mke wa Waziri Mkuu, Mama Mary Majaliwa (kulia) wakati wa hafla ya Mahafali ya 10 ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) leo tarehe 21/11/2019 jijini Dodoma. Katika mahafali ya hayo Rais Dkt. John Pombe Magufuli ametunukiwa Shahada ya heshima ya Udaktari wa Falsafa (Phd) katika Sayansi ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuleta maendeleo ya nchi.
  •  Rais Magufuli amewashukuru viongozi wote nchini, Chama Cha Mapinduzi (CCM), vyombo vya Ulinzi na Usalama, viongozi wa Dini, viongozi wa Siasa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano wao mkubwa katika kuhakikisha nchi inakua na amani na utulivu, na miradi ya maendeleo inatakelezwa kwa mafanikio makubwa.
  • Pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika maeneo mbalimbali ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imetilia mkazo, Rais Magufuli amewataka Watanzania wote kuendelea kushikamana katika kujenga nchi na kutokubali kuyumbishwa na changamoto za mabeberu na vibaraka wao waliopo ndani ya nchi, ambao wamekuwa wakitumika kukwamisha juhudi za Serikali katika maendeleo na safari ya kuufikia uchumi wa kati ifakapo mwaka 2025.
44-01
Rais Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza mara baada ya kutunukiwa Shahada ya heshima ya Udaktari wa Falsafa (Phd) katika wakati wa Mahafali ya 10 ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) leo tarehe 21/11/2019 jijini Dodoma. Rais Magufuli ametunukiwa PhD hiyo ikiwa ni kutambua mchango wake katika maendeleo ya nchi ambapo anakuwa mtu wa tatu kutunukiwa Shahada ya heshima ya Uzamivu na chuo hicho akitanguliwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete na Mzee Rashid Mfaume Kawawa.
  • Amewapongeza wahitimu wa UDOM wa mwaka huu na ametoa wito kwa wasomi hapa nchini kuendelea kufanya tafiti mbalimbali zinazojielekeza kutatua changamoto za Watanzania, na kwamba tafiti hizo zisiwe tegemezi kwa watu wa nje ambao ndio huchagua ajenda za utafiti huku akibainisha kuwa Serikali itaendelea kuchangia mfuko wa utafiti.
  • Kesho tarehe 22 Novemba, 2019 Rais Magufuli ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Uhuru katika eneo la Maduka Chamwino, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa nyumba 118 za askari polisi katika eneo la Nzuguni, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Dodoma katika eneo la Nzuguni, ataweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa Soko Kuu la Dodoma katika eneo la Nzuguni na kisha atazungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara.
Ad

Unaweza kuangalia pia

LIVE: UZINDUZI WA MAJENGO YA OFISI YA MANISPAA NA MKUU WA WILAYA KIGAMBONI JIJINI DSM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 11, Febuari, …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *