VIWANJA VYA NDEGE VYA SHINYANGA, KIGOMA, TABORA NA SUMBAWANGA KUJENGWA KWA VIWANGO VYA KIMATAIFA

Na. Ramadhani Kissimba na Peter Haule, Dar es Salaam

Serikali imezindua mradi wa ujenzi, ukarabati na upanuzi wa viwanja vinne vya ndege vya Shinyanga, Tabora, Sumbawanga na Kigoma ili viwe na kiwango cha kimataifa, utakaogharimu shilingi bilioni 136.85.

Ad

Akizindua ujenzi wa mradi huo jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James, amesema kuwa fedha hizo zimetolewa kama mkopo wenye masharti nafuu na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (European Investment Bank) kwa ajili ya kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji wa abiria katika maeneo hayo ya kimkakati.

‘’Nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Wadau wa Maendeleo hususan Benki ya Uwekezaji ya Ulaya kwa kukubali kufadhili mradi wa Viwanja vya Ndege vya kimkakati kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania’’Alisema Bw. James

Bw. Doto James alieleza kuwa uboreshaji wa viwanja hivyo vya kimkakati unalenga kuvipa uwezo viwanja vya ndege vya mikoa ya Shinyanga, Tabora, Sumbawanga na Kigoma ili kutumia fursa nyingi zilizopo kwenye maeneo hayo na kukuza uchumi ambao utakuwa chachu ya maendeleo katika Sekta ya Uchukuzi, Utalii, Kilimo na Anga katika mikoa husika na nchi kwa ujumla.

“Kukamilika kwa mradi huu kutaongeza uhakika wa kufikika, kurahisisha usalama, mawasiliano, na kuboresha biashara na nchi jirani na kuvifanya viwanja hivyo vitumike wakati wote kwa kuweka miundombinu ya taa na kuvipa hadhi ya Kimataifa ili ndege kubwa kama “Dreamliner” ziweze kutua” aliongeza Bw. James

“Ni matumaini ya Serikali kuwa utekelezaji wa miradi hii utakuwa chachu ya maendeleo katika Sekta ya Uchukuzi, Utalii, Kilimo na Anga katika mikoa husika na nchi kwa ujumla” alifafanua Bw. James

Alisema Kiwanja cha ndege cha Shinyanga kitajengwa kwa gharama ya dola za Marekani 19,087,558 (sawa na shilingi bilioni 44.07), Sumbawanga, dola za Marekani 21,699,083 (sawa na shilingi bilioni 50.11) Tabora, dola za Marekani 10,491,745 (sawa na shilingi bilioni 24.23), Kigoma kitajengwa kwa kutumia dola za Marekani 11,794,876.62 (sawa na shilingi bilioni 27.24) .

Aidha, Bw. James alifafanua kuwa gharama za washauri elekezi katika mradi huo ni dola za Marekani 2,208,803 (sawa na shilingi bilioni 3.69) kwa Viwanja vya ndege vya Shinyanga na Sumbawanga na dola za Marekani 1,599,034.30 (sawa na shilingi bilioni 3.69) kwa Viiwanja vya Ndege cha Kigoma na Tabora.

Bw. James aliwataka wakandarasi waliopewa kazi ya ujenzi wa viwanja hivyo ambao M/S China Henan International Corporation Group Ltd (Chico); M/S Sino- Shine Overseas Construction and Investment East Africa Limited; Beijing International Corporation Group C. Ltd).

Alimwagiza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS, Mhandisi Patrick Mfugale, kusimamia kwa karibu ujenzi wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati kwa mujibu wa mikataba waliyoingia na wakandarasi hao ambao ni kipindi cha kati ya miezi 12 na 18 na kwamba hakutakuwa na muda wa nyongeza.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS, Mhandisi Patrick Mfugale, alisema ujenzi wa viwanja hivyo utahusisha upanuzi wa njia za kurukia ndege, majengo ya abiria, barabara za lami za kuingia uwanjani na ujenzi wa maegesho ya magari.

Akizungumza kwa niaba ya wakuu wa Mikoa ya Kigoma, Tabora, Shinyanga na Rukwa ambao watanufaika na mradi huo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Bw. Rashidi K. Mchata, alisema kuwa ukamilishaji wa miradi hiyo utasaidia kuunganisha shughuli za uchumi katika mikoa ya pembezoni ya nchi kwa kuwa viwanja hivyo vitakuwa na uwezo wa kuwahudumia wananchi saa 24 kwa majuma 52 na siku 336 kwa mwaka.

Ad

Unaweza kuangalia pia

Mitazamo ya Uongozi ya Mhe. Ummy Ally Mwalimu katika Sekta za Afya, Maendeleo ya Jamii, na Haki za Watoto

Ummy Ally Mwalimu ameonyesha mitazamo ya uongozi yenye mwelekeo wa kujali maendeleo na ustawi katika …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *