RAIS WA ZANZIBAR DKT. MWINYI AKUTANA NA UJUMBE WA JUMUIYA YA MADHEHEBU YA BOHORA

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amewakaribisha wawekezaji kutoka Jumuiya ya Madhehebu ya Bohora kuja kuekeza Zanzibar kutokana na fursa mbali mbali zilizopo hapa nchini.

Rais Dk. Hussein Ali Mwinyi aliyasema hayo leo Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipokutana na Wajumbe wa Jumuiya ya Madhehebu ya Bohora kutoka Zanzibar na Tanzania Bara wakiongozwa na kiongozi wao Sheikh Tayabali Hamza Bhai Patanwalla ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya mwenye makao makuu yake Jijini Dar es Salaam.

Rais Dk. Hussein aliueleza Ujumbe huo wa Jumuiya ya Madhehebu ya Bohora kutoka Zanzibar na Dar-es Salaam kwamba milango ya Zanzibar iko wazi hivyo, anawakaribisha kuja kuekeza Zanzibar hasa ikizingatiwa kwamba walio wengi katika Jumuiya hiyo ni wafanyabiashara.

Alisema kuwa Zanzibar ina fursa nyingi za kuekeza katika sekta mbali mbali za maendeleo zikiwemo viwanda hivyo, aliwataka kuitumia fursa hiyo na kusisitiza kwamba iwapo itazitumia fursa hiyo vyema itasaidia katika kutoa ajira kwa vijana.

Ad

Aliongeza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Nane itaendelea kushirikiana na Madhehebu hayo pamoja na yale mengine yote hapa nchini katika kuhakikisha kunakuwepo mashirikiano ya pamoja kwa azma ya kuendeleza na kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Rais Dk. Hussein Mwinyi aliipongeza Jumuiya hiyo kwa kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha na kuendeleza sekta mbali mbali za kijamii, kiuchumi na kimaendeleo zikiwemo huduma za afya, elimu na nyenginezo.

Aidha, Rais Dk. Hussein Mwinyi alitoa shukurani kwa Kiongozi wa Madhehebu ya Bohora duniani Dk. Syedna Mufaddal Saifuddin kutokana na salamu zake za pongezi alizomletea ambazo ziliwasilishwa na viongozi hao katika mkutano wao huo hivi leo.

Akitoa shukurani kutokana na salamu hizo, Rais Dk. Mwinyi aliipongeza Jumuiya hiyo kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano uliopo na kuahidi kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Jumuiya hiyo bega kwa bega.

Ad

Unaweza kuangalia pia

Mitazamo ya Uongozi ya Mhe. Ummy Ally Mwalimu katika Sekta za Afya, Maendeleo ya Jamii, na Haki za Watoto

Ummy Ally Mwalimu ameonyesha mitazamo ya uongozi yenye mwelekeo wa kujali maendeleo na ustawi katika …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *