RAIS MAGUFULI AMFUTA MACHOZI MFANYABIASHARA ALIYEZUILIWA BIDHAA ZAKE TANGU 2015

 

  • Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kumlipa fidia mfanyabiashara ambaye bidhaa zake zilishikiliwa na Mamlaka hiyo tangu mwaka 2015 kinyume na taratibu.
  • Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo Juni 7, 2019 wakati akiongea na wafanyabiashara kutoka wilaya zote za Tanzania kwa lengo la kuangalia changamoto na fursa zilizopo katika kufanya biashara nchini.
MW
Mawaziri pamoja na Wafanyabiashara mbalimbali wakiwa katika kikao cha Wafanyabiashara Wakubwa kutoka katika Wilaya zote nchini pamoja na Wajumbe wa Baraza la Biashara la Taifa TNBC katika Ukumbi wa Kikwete Ikulu jijini Dar es Salaam.
  • Ametoa maagizo hayo baada ya Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa kuelezea namna alivyoingilia kati suala la mfanyabiashara huyo wa Kariakoo (jina lake halikujulikana mara moja) kurejeshewa bidhaa zake zilizokuwa zimezuiliwa baada ya mfanyabiashara huyo kukataa kutoa rushwa kwa Maafisa watatu wa TRA.
  • “Hao watatu wote Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU kawashike na uwaweke ndani halafu wapelekwe Mahakamani, wakiwa Mahakamani Kamishna Mkuu wa TRA uwe umewasimamisha kazi, lakini TRA mkapige hesabu ile biashara yake imekaa kwa miaka mitatu mkamlipe fidia,” Rais Magufuli alitoa maagizo.
MW
Wafanyabiashara Wakubwa kutoka katika Wilaya mbalimbali nchini wakichangia hoja mbalimbali katika Kikao chao na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam.
  • Aidha, Rais amewataka wafanyabiashara kuiga mfano wa mfanyabiashara mwenzao aliyekataa kutoa rushwa na kuwaomba watoe ushirikiano katika kulipa kodi na pia Mamlaka ya Mapato kutomuonea mfanyabiashara katika kumkadiria kodi.
  • Waziri Mkuu alikuwa akielezea malalamiko aliyopata kutoka kwa wafanyabiashara hususani kodi kubwa na rushwa ambapo baadhi ya maofisa wamekuwa wakitumia vibaya majina ya viongozi kwa kusingizia kuwa ni maagizo kutoka juu.
  • Mheshimiwa Kassim Majaliwa alieleza kwamba aligundua matatizo hayo baada ya kutembelea eneo la biashara la Kariakoo jijini Dar es Salaam na kugundua mfanyabishara mmoja aliingia na bidhaa kutoka Zambia na kuwa na vibali vyote lakini alipofika Kimara alizuiliwa na kuomba rushwa lakini Mfanyabiashara huyo alikataa kutoa rushwa na TRA wakachukua bidhaa zake kupeleka bohari.
P
Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Biashara la Taifa TNBC pamoja na Wafanyabiashara Wakubwa kutoka katika Wilaya zote nchini wakiwa katika Kikao na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam.
  • Kwa upande wake Waziri Mkuu amewataka wafanyabishara kuendelea kuwa na imani na Serikali ina haki na wajibu wa kuwalinda wafanyabishara kwa namna yeyote ile na ndio maana Serikali inachukua hatua mbalimbali ili kuweka mazingira bora kwa wafanyabishara.
  • Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa Serikali itahakikisha inajenga mazingira wezeshi nchini na pia itaimarisha biashara za mipakani na pia eneo la Kariakoo ambalo ndio soko kubwa ambapo wafanyabishara kutoka Malawi, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamekuwa wakichukua bidhaa Kariakoo.
  • Mkutano wa Rais na wafanyabiashara kutoka wilaya zote mchini uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam pia ulihudhuriwa na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Katibu Mkuu Kiongozi, Mawaziri, Makatibu Wakuu na baadhi ya Wakuu wa taasisi za Serikali na sekta binafsi.
Ad

Unaweza kuangalia pia

WAZIRI MKUU MAJALIWA AZUNGUMZA NA BODI YA NHC

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *