Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, akisalimiana na mwekezaji wa Kiwanda cha Madawa cha Vista Pharma Ltd wakati wa ziara yake ya kuangalia maendeleo ya viwanda vya kutengeneza dawa mkoani Kibaha.

WAZIRI UMMY AWAPONGEZA WAWEKEZAJI VIWANDA VYA DAWA – KIBAHA

  • Waziri wa Afya, Ustawi  wa Jamii, Jinsia,Wazee  na Watoto, Ummy  Mwalimu, amesema katika kila Sh. 100 ambayo Serikali inatumia kununua dawa nchini, Sh. 94 inapelekwa nje ya nchi kwa ajili ya ununuzi wa dawa hizo.
  • Waziri Ummy alisema hayo jana wilayani Kibaha, Pwani wakati wa ziara yake ya kutembelea na kuangali maendeleo ya ujenzi wa Viwanda vya dawa ambavyo ni Kampuni ya Kairuki Pharmaceutical Industrial Limited (KPIL) na Vista Pharma Ltd.
JENGO
Moja ya majengo ya ofisi katika kiwanda cha Vista Pharma.
  • Alisema fedha hiyo inayokwenda nje kwa ajili ya ununuzi wa dawa ni kubwa na ili kuikoa ni muhumu kwa wawekezaji kuendelea kuwekeza nchini hasa katika ujenzi wa viwanda vikiwemo vya dawa na vifaa tiba ambavyo ndivyo vinapewa kipaumbele na serikali.
  • “Changamoto tunayopitia Serikali mbali na kwamba tunatumia fedha nyingi katika uagizaji wa dawa, bado dawa hizi zinachelewa kufika, Bohari ya Dawa (MSD) imekuwa ikiagiza dawa nje ya nchi na dawa hizo hukaa takribani zaidi ya miezi sita ndio zinaingia nchini, jambo hili ufanya upatikanaji wa dawa usiwe rahisi.
  • “Hivyo tunaposema upo umuhimu wa ujenzi wa viwanda vya dawa tunamaanisha,” alisema.
WAZIRI WA AFYA
Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, akiangalia ramani ya ujenzi wa Kiwanda cha Kairuki Pharmaceutical Industrial Limited (KPIL).
  • Alisema ujenzi wa viwanda nchini utasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza gharama za uagizaji wa dawa hizo nje ya nchi, gharama za upatikanaji wa dawa nchini kushuka na kuokoa fedha zinazonunulia dawa hizo.
  • “Kati ya wadau 72 wa masuala ya afya nchini walioomba kujenga viwanda vya dawa hapa nchini, ni nane mpaka sasa ndio wameanza kujenga na kati ya hao sita viwanda vipo Kibaha.
KIWANDA
Kiwanda cha Vista Pharm kikiwa katika hatua za awali za ujenzi wake.
  • “Hii inaonyesha ni kwa namna gani viwanda hivi vikikamilika vitakavyozalisha dawa zenye ubora zaidi na kuhakikisha tunaokokoa fedha za nje tunazozitumia katika kununua dawa,” alisema na kuongeza “Kwa mwaka huu wa fedha serikali imetenga Sh. Bilioni 270 katika wizara yangu kutoka Sh. Bilioni 30, hivyo fedha za kununua dawa zipo wawekezaji wakazane wamalize haraka viwanda hivyo  ili fedha hizi zibaki hapa nchini, ” alisema.
  • Hata hivyo, alisema serikali  itahakikisha inatengenza mazingira mazuri ya kurahisisha ujenzi wa viwanda  unaenda sambamba na uimarishaji wa miundombinu ya umeme, maji na barabara.
WAZIRI WA AFYA
Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akiwa katika ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kiwanda cha Madawa cha Kairuki, kilichopo Kibaha mkoani Pwani.
  • Kwa Upande wake, Msimamizi wa Kiwanda cha Kairuki, Dk.Mganyizi Kairuki, alisema kiwanda chao kinatarajia kuanza uzalishaji wa dawa za maumivu na nyingine aina 10 ambazo ni za maji ifikapo mwakani.
  • Alisema mbali na uzalishaji wa dawa, kiwanda hicho pindi kitakapokamilika  kinatarajia kutoa ajira za moja kwa moja 200 na zisizo za moja kwa moja 1,000. “Zaidi ya Sh. Bilioni 38 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa kiwanda hiki fedha ambazo ni mikopo kutoka benki, hivyo tunazidi kuziomba baadhi ya benki kukopesha maana suala hili limekuwa ni changamoto,” alisema.
OFISA MTENDAJI
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Madawa cha Vista Pharm, Churchil Katwaza, akisoma taarifa za kiwanda hicho kwa Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu.
  • Naye Mwenyekiti wa Kampuni ya Bandari Pharmacy inayojenga kiwanda cha Vista Pharmacy, Churchill Katwaza, alisema kiwanda chao kinatarajia kuzalisha dawa sita ikiwemo ya kutuliza maumivu ya tumbo, kuongeza damu kwa wajawazito pamoja na inayotibu ushambulizi wa vidudu vya bakteria mwilini.
  • “Tutazalisha jumla ya vidonge milioni 702 kwa mwaka na takribani chupa milioni 32 za dawa ya maji zenye ujazo wa milimita 100,”alisema Katwaza.
Ad

Unaweza kuangalia pia

ONGEZENI KASI YA KUWAHUDUMIA WANANCHI – DKT. CHAULA

Watumishi wa afya nchini wametakiwa kuongeza kasi ya kuwahudumia wananchi kwenye vituo vya kutolea huduma …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *