NAIBU WAZIRI SIMA AAGIZA WACHIMBAJI WADOGO KUSAJILIWA

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Sima akiongea na Mkuu wa Wilaya ya Songwe Bw. Samuel Jeremia Opulukwa (wa pili kushoto) wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua shughuli za uhifadhi wa Mazingira katika Wilaya hiyo. Kulia ni Prof Esnat Chaggu Mwenyekiti wa Bodi – Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC na Dkt. Samuel Gwamaka Mkurugenzi Mkuu – NEMC.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima ameuagiza uongozi wa Wilaya ya Songwe kuwabaini, kuwasajili na kuunda vikundi vya wachimbaji wadogo wasio rasmi ili waweze kutambulika na kufaidika na mikopo midogo midogo inayotolewa na Serikali hapa nchini.

Ameyasema hayo hii leo mara baada ya kufanya ziara ya kikazi katika Mkoa wa Songwe hususan Wilaya ya Songwe na kubaini changamoto ya wachimbaji wadogo wanaoharibu mazingira kutokana na uchimbaji holela.

Ad

“Ni lazima mchukue hatua za haraka za kuwatambua wachimbaji hawa kwa lengo la kuwasajili na kuanzisha kanzi data itakayosaidia katika zoezi la utoaji wa elimu ili kunusuru mazingira” Sima alisisitiza.

Waziri Sima amesisitiza kuwa ni vema pia Wilaya ya Songwe ikaanzisha vikundi vya mazingira na kuhamasisha matumizi ya Sheria ndogondogo katika maeneo yao.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Sima akitoa maelekezo kwa Bw Honest Mrema Meneja Mkuu wa Mgodi wa Shanta mara baaada ya Naibu Waziri Sima kutembelea mgodi huo kukagua bwawa la kuhifadhi tope sumu litokanalo na uchenjuaji wa dhahabu mgodini hapo.

Akiwasilisha taarifa ya hali ya Mazingira katika Wilaya hiyo Mkuu wa Wilaya ya Samuel Jeremia Opulukwa amesema Wilaya yake inakabiliwa na changamoto kubwa za uchomaji wa misitu unaohatarisha maisha ya viumbe hai na ikolojia ya eneo hilo.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samuel Gwamaka ametoa wito kwa watafiti wa madini katika eneo hilo kutoa taarifa rasmi katika ngazi ya Wilaya ili kuepuka uharibifu wa mazingira unaofanywa na watafiti hao kwa kuchimba kiholela kwa lengo la kutafuta dhahabu.

Pia, Naibu Waziri Sima ametembelea Mgodi wa Shanta na kuagiza uongozi wa mgodi huo kutoa elimu kwa jamii inayozunguka mgodi huo juu ya namna bora ya uchimbaji wa madini kwa njia bora na salama kwa mazingira.

“Kwa kuwa mgodi huu unatumia teknolojia ya kisasa zaidi, natoa rai kwa mgodi kuhamisha teknolojia hii kwa wachimbaji wadogo wadogo ili wananchi pia wanufaike” Sima alisisitiza.

Mheshimiwa Mussa Sima yuko Mkoani Songwe kwa ziara ya kikazi na ametembelea Wilaya ya Songwe na kukagua usimamizi na uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira ambapo kesho atawasili Mkoani Mbeya.

Ad

Unaweza kuangalia pia

Mitazamo ya Uongozi ya Mhe. Ummy Ally Mwalimu katika Sekta za Afya, Maendeleo ya Jamii, na Haki za Watoto

Ummy Ally Mwalimu ameonyesha mitazamo ya uongozi yenye mwelekeo wa kujali maendeleo na ustawi katika …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *