BENKI YA MAENDELEO YA AFRIKA KUSAIDIA UJENZI WA MIRADI YA NISHATI TANZANIA

  • BENKI ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) imeahidi kuendelea kuisadia Tanzania kutekeleza miradi yake mikubwa ya kimkakati hususan miundombinu ya Nishati na Barabara kwa kuendelea kuipatia mikopo yenye masharti nafuu ili kuharakisha maendeleo ya nchi.
  • Ahadi hiyo imetolewa Mjini Johannesburg nchini Afrika ya Kusini na Kaimu Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayesimamia Miundombinu ya nishati, Bw. Wale Shonibare alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango, kando ya Kongamano la Pili la Jukwaa la Uwekezaji Afrika lililoandaliwa na Benki hiyo.
1-01
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kushoto), akiwa na Kaimu Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayehusika na miundombinu ya Nishati Bw. Wale Shonibare, baada ya kufanya mazungumzo kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Benki hiyo, Jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
  • Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa mkutano wao, Dkt. Mpango amesema kuwa ameiomba Benki hiyo kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya kipaumbele inayojengwa na Serikali hususan katika Sekta za nishati, barabara, uongezaji thamani wa mazao ya kilimo, elimu na maji.
  • Dkt. Mpango ameitaja miradi iliyowasilishwa kwa kiongozi huyo kuwa ni mradi wa kuzalisha umeme wa Ruhudji (MW 358), mradi wa umeme wa Rumakali (MW 222) mradi wa umeme wa mto Malagarasi (MW 44.5), Mradi wa kuzalisha umeme wa Kakono (MW 87) na miradi mingine ambayo itajadiliwa na Bodi ya Benki hiyo itakayokutana mwishoni mwaka huu.
3-01
Kaimu Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayehusika na miundombinu ya Nishati Bw. Wale Shonibare (kulia) akiwa na mmoja wa Mkurugenzi wa Benki hiyo Bw. Baldeh Batchi, wakiandika maelezo yaliyokuwa yakitolewa na Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (hayupo pichani) walipokutana Jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
  • Amesema kuwa miradi hiyo mikubwa itakayoiwezesha nchi kuwa na umeme wa kutosha ni muhimu kwani itasaidia kufanikisha agenda ya Seikali ya kuwa na uchumi wa kati wa viwanda ifikapo mwaka 2025.
  • “Tumewakaribisha waje Tanzania kwa ajili ya mazungumzo na kujionea namna miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo vingine kama umeme jua na ule unaozalishwa kwa njia ya upepo kama ilivyo katika maeneo mengine ya Afrika hususan Kusini mwa Jangwa la Sahara” alisisitiza Dkt. Mpango
  • Amesema kuimarika kwa Sekta ya nishati nchini kutaleta manufaa makubwa ikiwemo kuziwezesha biadhaa za kilimo kama vile pamba kuongezewa thamani kutokana na kuwepo kwa umeme wa uhakika wa kuendesha viwanda.
4-01
Kaimu Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayehusika na miundombinu ya Nishati Bw. Wale Shonibare akisikiliza kwa makini maelezo yaliyokuwa yakitolewa na Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (hayupo pichani) walipokutana Jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
  • Kwa upande wake Kaimu Makamu wa Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Bw. Wale Shonibare, amesema kuwa Benki yake iko tayari kuisaidia Tanzania ili ifikie mapinduzi makubwa ya miundombinu ya nishati kutokana na umuhimu wake katika kuendesha uchumi.
  • Alisema nishati ni jambo muhimu ili nchi iweze kufikia mapinduzi ya viwanda na aliahidi kufanya kila linalowezekana kuhakikisha Benki yake inachangia juhudi za serikali za kuongeza uwezo wa kuzalisha umeme, kujenga njia za kusafirishia umeme na usambazaji wake kwa kulijengea uwezo Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO).Na Benny Mwaipaja, Johannesburg
Ad

Unaweza kuangalia pia

WAKAZI WA PEMBEZONI MWA BAHARI WAELIMISHWA ATHARI ZA MAGENDO

Wakazi na wafanyabiashara waishio pembezoni mwa fukwe za Bahari ya Hindi katika kata za Somangila, …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *