NI MRADI WA UMEME WA MTO RUFIJI SIYO STIEGLER’S – WAZIRI KALEMANI

  • Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, amewasihi watanzania kuwa wazalendo kwa kuacha kuuita mradi wa kuzalisha umeme kwa maporomoko ya maji ya mto Rufiji kwa jina la Stiegler’s badala yake wauite kwa jina lake halisi la kizalendo.
  • Aliyasema hayo kwa nyakati tofauti jana, Julai 24, 2019 wakati akizungumza na waandishi wa habari mkoani Morogoro na baadaye akiwa Rufiji mkoani Pwani mara baada ya kutembelea na kukagua maandalizi ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa mradi huo, unaotarajiwa kufanywa na Rais John Pombe Magufuli, kesho, Julai 26.
  • “Jina halisi ni Mradi wa Umeme wa Rufiji na siyo Stiegler’s kama ambavyo wengi wamekuwa wakiuita. Nawasihi watanzania kuenzi jina la utaifa la Rufiji,” alisisitiza Waziri.
RU 2-01
Matukio mbalimbali wakati Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani alipokuwa akikagua maandalizi hafla ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rufiji, unaotarajiwa kufanyika Julai 26, 2019.
  • Akizungumza katika maeneo hayo tajwa, Dkt. Kalemani alisema utekelezaji wa mradi husika, utaweka mazingira sahihi, yanayotabirika na imara katika kujenga uchumi wa viwanda.
  • Akifafanua, alisema hiyo ni kutokana na Sera na Dira ya Taifa ya kujenga uchumi wa viwanda, lakini pia kuinua maisha ya watanzania kutoka kima cha chini kwenda kima cha kati ifikapo mwaka 2025.
  • Alisema, lengo kubwa la mradi husika; pamoja na mambo mengine, ni kuzalisha umeme wa kutosha, wa uhakika, unaotabirika na wenye gharama nafuu.
RU 3-01
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani akizungumza na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali mkoani Morogoro, kuhusu maandalizi ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rufiji, unaotarajiwa kufanyika Julai 26, 2019.
  • “Tumpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa umahiri mkubwa wa utekelezaji wa mradi huu. Kwa niaba ya Wizara ya Nishati, nataka kuwahakikishia watanzania kuwa mradi huu utatekelezeka kwa wakati na upo uwezekano wa kuokoa walau mwezi mmoja wa ukamilishaji wake kimkataba.”
  • Akizungumzia manufaa makubwa mengine ya mradi, alisema ni pamoja na ajira ambapo alieleza kuwa hadi sasa watanzania 600 wameajiriwa kwa shughuli za awali za ujenzi. Aliongeza kuwa, idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka kufikia 6,000 na zaidi pindi mradi utakapofikia katika kilele cha ujenzi wake.
  • Waziri alieleza manufaa mengine kuwa ni uunganishaji wau meme katika maeneo yaliyo jirani na mradi ambapo alisema jumla ya vijiji 22 vya mikoa ya Morogoro na Pwani tayari vimeshanufaika na kwamba vijiji vingine 37 vya mikoa hiyo vitapatiwa umeme baada ya kujenga miundombinu ya kuusafirisha.
RU 4-01
Baadhi ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), wakifuatilia mkutano wa Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani) na waandishi wa habari wa Morogoro (hawapo pichani) kuhusu maandalizi ya hafla ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa mradi wa umeme wa Rufiji, unaotarajiwa kufanyika Julai 26, 2019.
  • Vilevile alitaja manufaa mengine kuwa ni pamoja na kuwezesha kilimo cha umwagiliaji, uvuvi pamoja na kuwezesha uhifadhi wa mazingira kutokana na kupunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya mkaa yanayosababisha ukatwaji wa miti.
  • Aliwaasa wananchi kufanya utalii wa ndani kwa kutembelea eneo la mradi ili kujionea na kujifunza, kabla watalii kutoka nchi mbalimbali duniani hawajaanza kuja kutalii eneo hilo.
  • Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Stephen Kebwe alimpongeza Waziri wa Nishati kwa jitihada ambazo Wizara imeendelea kufanya katika utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa umeme wa Rufiji.
RU 5-01
Matukio mbalimbali wakati Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani alipokuwa akikagua maandalizi hafla ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rufiji, unaotarajiwa kufanyika Julai 26, 2019.
  • Alisema mradi utaleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Morogoro kama yalivyoelezwa na Waziri lakini pia akamhakikishia Dkt. Kalemani kuwa suala la ulinzi na usalama katika eneo la mradi limezingatiwa kwa uzito wa aina yake.
  • “Tumeongeza idadi ya askari Polisi ili kudhibiti kikamilifu tukio lolote la kihalifu endapo litajitokeza. Hata hivyo, hadi sasa hatujapata shida yoyote ya kiusalama,” alisema.
  • Mkutano wa Waziri na waandishi wa habari ulihudhuriwa pia na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, Mkurugenzi wa Idara ya Habari – MAELEZO, Dkt Hassan Abbas pamoja na wataalamu mbalimbali wa Wizara na TANESCO.Na Veronica Simba – Pwani
Ad

Unaweza kuangalia pia

TPDC YAOKOA TRILIONI 12.7 KUAGIZA MAFUTA NJE YA NCHI

Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *