MRADI WA PERI URBAN KUKAMILIKA KWA WAKATI

Hafsa Omar-Dodoma

Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Leonard Masanja amewataka wakandarasi wanaotekeleza mradi wa Umeme katika Vijiji vilivyo pembezoni mwa Mji (Peri-Urban) kukamilisha utekelezaji wa miradi yao ndani ya muda uliopangwa.

Ad

Ameyasema hayo,Agosti 19,2020,wakati alipokuwa kwenye kikao na  Wakandarasi  wa mradi wa Per-Urban, kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Nishati, Mkoani Dodoma.

Katika kikao hicho,kilihudhuriwa na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Edward Ishengoma, Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga,Kamishna Msaidizi Maendeleo ya Umeme Mhandisi Styden Rwebangila,Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO) Dkt Tito Mwinuka na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijiji(REA) Mhandisi Amos Maganga.

Aidha,amesema mradi huo ambao unatarajiwa kukamilika Septemba 15,mwaka huu,wakandarasi hao hawataongezewa muda kwakuwa Serikali ilitoa muda wa kutosha kutekeleza mradi huo.

Ameongeza kuwa, wakandarasi wote walikubaliana na Serikali kuwa watafuata masharti yote ya mikataba waliosaini na kuwataka kufuata miongozo yote ya  mikataba hiyo ili kukamilisha kazi hiyo.

“Hii miradi ya peri-urban inatekelezwa sehemu ambazo watu wana uhitaji mkubwa wa umeme,ni Sehemu ambazo shughuli za kiuchumi zipo nyingi, watu wanahitaji maendeleo bila ya umeme kuna shughuli za kiuchumi zitakwama kwahiyo tujitahidi kumaliza miradi hii kwa wakati,”alisema.

Amesema, Serikali haitawavumiliana tena kwakuwa ilitoa mda wa kutosha kwa wakandarasi hao kufanya kazi zao katika maeneo yao na kinachotakiwa kwasasa ni kukabidhi miradi kwa wakati.

Aidha, aliwataka wakandarasi hao kufanya kazi kwa uzalendo kwakuwa,Serikali iliamua kuwapa kipaumbele wakandarasi wa ndani na kutochukua wakandarasi kutoka nje kwa kuona kuwa  kampuni tulizonazo nchini zinauwezo wa kufanya kazi hizo.

Alifafanua kuwa, Serikali imeamua kuweka mikakati ya makusudi ili  kujewajengea wananchi wake uwezo ,na ndio ikamua kwenye miradi hii itumie wakandarasi wazawa na iliamua kulegeza masharti  kwa makusudi ili mikataba ichukuliwe na  kampuni za kwetu.

Pia, amewaeleza vigezo ambavyo vitatumika kwenye upatikanaji wa kazi za miradi mengine ya umeme, ambapo amesema moja ya kigezo cha kupewa kazi nyengine ni pamoja na utendaji wa kazi mzuri kwenye miradi mengine  ya umeme iliyopita na kuwataka kufanya kazi kwa weledi ili waweze kupata kazi nyengine.

Nao,wakandarasi wa mradi huo, waliohudhuria kikao hicho ambao ni Sinotec Co.LTD, Ceylex Engineering LTD, Sengerema,Namis Corporate LTD na Derm Electrics LTD, kwa pamoja walisaini makubaliano ya kumaliza kazi ya miradi hiyo kwa muda uliopangwa.

Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Edward Ishengoma,amesema Serikali itawasimia wakandarasi hao ili kuhakikisha wanafanya kazi kimamilifu na wanamaliza kazi zao ndani ya muda uliopangwa.

Naye, Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi Innocent Luoga,amewataka wakandarasi hao kuelekeza nguvu zao zote katika kukamilisha miradi hiyo na kufanya kazi kwa bidi ili miradi hiyo imalizike kwa wakati uliopangwa.

Ad

Unaweza kuangalia pia

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA MKUTANO WA WOMENLIFT HEALTH

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango akimsikiliza Maelezo kutoka kwa …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *