WAZIRI MKUU ASHUHUDIA MV KILINDONI IKIWEKWA MAJINI

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya tano itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha inatekelezwa kwa viwango na kuwanufaisha watumiaji.

Waziri Mkuu amesema hayo (Jumanne, Desemba 15, 2020) wakati aliposhuhudia uingizwaji majini wa Kivuko cha MV Kilindoni ‘Hapa kazi Tu’ kitakachofanya safari zake kati ya Nyamisati na Mafia, tukio hilo limefanyika Karakana ya Kujenga na Kukarabati vivuko ya Songoro iliyopo Kigamboni, jijini Dar es salaam

Ad

Waziri Mkuu amesema kuwa ujenzi wa kivuko hicho unatokana na ustashi wa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kuhakikisha kwamba ahadi zote zilizowekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya Mwaka 2020-2025 ili Watanzania waweze kuthibitisha kuwa CCM inaahidi na kutekeleza.

“Kwenye Ilani ya 2015-2020, Chama cha Mapinduzi kilisema na kuandika kwamba kutakuwa na kivuko cha kwenda Mafia, hii hapa leo inaingia majini tukiishuhudia kuelekea mafia.”

Aidha, Waziri Mkuu alisema kuwa katika kuhakikisha sekta ya majini inaimarishwa, Serikali imepanga kujenga meli itakayokuwa inafanya kazi katika ukanda wa bahari kutoka bandari ya Mtwara kupitia bandari ndogondogo za Lindi, Kilwa kuja Dar es Salaam, Tanga, Zanzibar pamoja na visiwa jirani vya Comoro.

Waziri Mkuu alifafanua kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha inaimarisha sekta za usafirishaji za barabara, anga, majini pamoja ya reli ili kuwawezesha Watanzania kuchagua aina ya usafiri wanaoutaka.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Umeme na Ufundi Serikalini (TEMESA), Mhandisi Japhet Masele alisema kuwa wakala huo katika mwaka wa fedha 2019-2020 ilikuwa inatekeleza ujenzi wa vivuko vinne na mpaka sasa vivuko vitatu vya MV Ilemela, MV Kayenze na MV Ukara vimeanza kutoa huduma huku MV Kilindoni ndio kimeingia majini kwa mara ya kwanza.

Amesema kuwa Kivuko kipya cha MV Chato kimekamilika na kinatarajiwa kuanza kazi baada ya ukaguzi wa mwisho unaoendelea kufanywa sasa na wataalam kutoka DMI na TASAC.   

Kwa upande wake, Naibu Waziri Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Mbunge wa Mafia, Mhe. Omary Juma Kipanga amesema kuwa anamshukuru Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwaheshimisa Wana-Mafia kwa kuhakikisha wanapata usafiri wa uhakika na salama.

Kivuko hicho cha MV Kilindoni kitakuwa na uwezo wa kubeba tani 100, yaani abiria 200, magari madogo sita.

Ad

Unaweza kuangalia pia

Mitazamo ya Uongozi ya Mhe. Ummy Ally Mwalimu katika Sekta za Afya, Maendeleo ya Jamii, na Haki za Watoto

Ummy Ally Mwalimu ameonyesha mitazamo ya uongozi yenye mwelekeo wa kujali maendeleo na ustawi katika …

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *