TANZANIA INASHIKA NAMBA MOJA KWA KUWA NA SIMBA WENGI BARANI AFRIKA

Yapongeza juhudi za Serikali katika kukomesha ujangili
Yazishauri nchi za Afrika kulinda na kuhifadhi wanyamapori
  • AFRICAN Wildlife Foundation imesema Tanzania ndio nchi inayoongoza kwa kuwa na Simba wengi na kwa upande wa Tembo inashika nafasi ya tatu barani Afrika.
  • Imesema hiyo inatoka na juhudi ambazo zinafanywa na Serikali ya Tanzania kuhakikisha wanyamapori na uhifadhi wa misitu unapewa kipaumbele.
  • Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Ofisa Mtendaji Mkuu wa African Wildlife Foundation Kaddu Sebunya wakati akizungmzia umuhimu wa uhifadhi wa wanyamapori na uhifadhi wa mazingira kwa nchi za Bara la Afrika.
  • “Serikali ya Tanzania ni mfano wa kuigwa katika eneo hilo la uhifadhi wa misitu na utunzaji wa wanyamapori. Hii imefanya katika nchi za Bara la Afrika ,Tanzania kushika nafasi ya kwanza kwa kuwa na Simba wengi na na inashika nafasi ya tatu kwa kuwa na tembo wengi. Nchi inayoongoza kwa kuwa na tembo wengi ni Botswana ikifuatiwa na Zimbabwe,”amesema Sebunya.
  • Amesisitiza ni muhimu wa kila nchi barani Afrika kuweka mikakati itakayosaidia maliasili zilizopo kutunzwa na kulindwa vema huku akieleza kwa sasa kuna changamoto ya wanyamapori wengi hasa Simba na Tembo kupungua.
SIMBA
Simba
  • “Ukweli Simba na Tembo wameendelea kupungua barani Afrika na sababu yake ni uwepo wa majangiri na uwindaji haramu.Hivyo African Wildlife Foundation tunahamasisha kila nchi kuweka mipango ambayo itasaidia kuwafanya Simba na Tembo waendelee kuwepo,”amesema.
  • Amesema kila nchi ikiamua hakuna ambacho kitashindikana ambapo ametoa mfano kwa Serikali ya Awamu ya Tano namna ilivyofanikiwa kudhibiti majangiri ukilinganisha na miaka ya nyuma.
  • “Katika hili la kulinda wanyamapori na uhifadhi kila nchi ikiamua inaweza.Niitolee mfano Tanzania miaka ya nyuma Tembo walikuwa wanauliwa sana lakini leo hii tembo hao hao wako salama kutokana na hatua ambazo Serikali inachukua,”amesisitiza.
  • Sebunya amesema watu wa Bara la Afrika wana maisha yao na tamaduni zao ambazo kimsingi zilizingatia uhifadhi wa misitu, mapori na wanyama lakini kadri siku zinavyokwenda na kuingia kwa tamaduni za nchi nyingine kumesababisha kuibuka kwa changamoto ambazo iko haja ya kuzikabili.
tembo
Tembo
  • “Katika nchi nyingi sana barani Afrika nusu ya wanyama walikuwa siku za nyuma leo hawapo.Hivyo tutaendelea kuzihamasisha nchi za Afrika kuweka kipaumbele katika eneo hilo.
  • “African Wildlife tumekuwa tukifanya jitihada za kuhamasisha wadau kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wanyama.Ndio maana hata kile Chuo cha Mwika ni sehemu ya mchango wetu. Watalaamu wengi uhifadhi wa mazingira , misitu na wanyamapori waliopo barani Afrika wamepikwa katika chuo hicho,”amesema Sebunya.
  • Wakati huo huo Sebunya amesema kadri nchi zinapofanya maendeleo ni vema pia zikazingatia utunzaji wa mazingira.”Nchi za Afrika zinahitaji kuwa na maendeleo na wakati huo huo zinapaswa kulinda mazingira.Ni mambo mawili yanayokwenda kwa pamoja,”amesema Sebunya.Na Said Mwishehe,Globu ya jamii
Ad

Unaweza kuangalia pia

WAZIRI ZUNGU AHUDHURIA MKUTANO WA 7 WA BARAZA LA KISEKTA LA MAWAZIRI WA MAZINGIRA NA MALIASILI WA JUMUIA YA AFRIKA MASHARIKI

             

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *