- Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, chini ya Mwenyekiti, Mariamu Ditopile Mzuzuri, imeipongeza Serikali kwa kutekeleza mradi wa umeme wa Makambako- Songea (kV 220) ambao umewezesha Mikoa ya Ruvuma na Njombe kupata umeme wa uhakika kutoka Gridi ya Taifa.
- Kamati hiyo, imetoa pongezi hizo wilayani Songea, Mkoa wa Ruvuma, baada ya kukagua utekelezaji wa mradi huo ambao umehusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kV 220 kutoka Makambako hadi Songea, ujenzi wa Vituo vya kupoza umeme vya Makambako, Madaba na Songea na usambazaji umeme katika Vijiji 122.
- Kabla ya kukagua kituo cha kupoza umeme cha Songea, Kamati hiyo ilikagua vituo vya Makambako na Madaba pamoja na njia ya usafirishaji umeme kutoka Makambako hadi Songea ambapo watendaji mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), walihudhuria.
- Awali, katika kituo kupoza umeme cha Makambako, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani aliieleza Kamati hiyo kuwa, mradi huo umekamilika mwaka 2018 na kazi inayoendelea sasa ni usambazaji wa umeme katika Vijiji vya awali 122 ambapo Vijiji 105 tayari vimeshaunganishwa na nishati hiyo.
- Dkt. Kalemani aliongeza kuwa, mradi huo umetekelezwa na Serikali ya Tanzania kupitia TANESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida) ambapo jumla ya gharama za mradi ni shilingi bilioni 216 na jumla ya wateja wa awali 22,000 watafaidika na mradi huo.
- Kwa upande wake, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, alisema kuwa, miundombinu hiyo ya usafirishaji umeme (kV 220) imejengwa kwa umbali wa kilomita 250 na jumla ya nguzo (Tower erection) 711 zimesimikwa.
- Aliongeza kuwa, kufika kwa umeme wa Gridi katika mikoa hiyo, kumefanya wananchi wahamasike kutumia umeme huo na kutoa mfano kuwa, awali matumizi ya umeme kwa Mkoa wa Ruvuma yalikuwa ni takriban megawati 9 lakini sasa yameongezeka na kufikia megawati 11 huku kazi ya kuwasambazia umeme wananchi ikiendelea.
Ad