RAIS DKT. MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA MRADI WA KUFUA UMEME WA MAJI KATIKA MTO RUFIJI

  • Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 26 Julai, 2019 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme katika mto Rufiji Mkoani Pwani ambao utakamilika Juni 2022 na kuzalisha megawati 2,115.
  • Sherehe za uwekaji wa jiwe la msingi la mradi huo zimefanyika kando ya eneo litakapojengwa bwawa la maji na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Waziri wa Nishati wa Misri Mhe. Dkt. Mohamed Shaker, Mawaziri na Naibu Mawaziri wa Tanzania, Wabunge, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, Viongozi wa Dini, Viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa taasisi mbalimbali za Serikali.
MG 1-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwasalimia viongozi mbalimbli mara baada ya kuwasili katika eneo la Mradi.
  • Ujenzi wa mradi huo utagharimu shilingi za Kitanzania Trilioni 6.5 na bwawa litakalojengwa litakuwa la kwanza kwa ukubwa Afrika Mashariki na la nne kwa ukubwa Barani Afrika, na Mhe. Rais Magufuli amependekeza bwana hilo liitwe Bwawa la Nyerere ikiwa ni kutambua na kuenzi maono ya Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere aliyetaka kujenga bwawa hilo wakati wa uongozi wake.
  • Katika hotuba yake, Mhe. Rais Magufuli ameipongeza Wizara ya Nishati kwa kusimamia utekelezaji mradi huo na ameeleza kuwa Serikali imechukua hatua za kujenga bwawa hilo ili kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kutoka megawati 1,601 zinazozalishwa hivi sasa, hadi kufikia megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025.
MG 2-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Waziri wa Nishati wa Misri Dkt. Mohamed Shaker, Waziri wa Nishati Medard Kalemani pamoja na viongozi wengine akisikiliza namna mradi wa Kuzalisha umeme Megawati 2115 katika eneo la mto Rufiji utakavyokuwa ukifanya kazi mara baada ya kukamilika.
  • Mhe. Rais Magufuli amesema pamoja na kutekeleza mradi huo, Serikali itajenga mradi wa kuzalisha umeme katika mto Ruhudji utakaozalisha megawati 359, mradi wa Lumakali megawati 222, mradi wa kakono megawati 87, Rusumo megawati 80 na mingine itakayotumia nishati ya gesi, makaa ya mawe, jua, jotoardhi, upepo na urani.
  • Amewataka wakandarasi wanaojenga mradi (Arab Contractors na Elsewedy Electric za Misri) kukamilisha mradi huo kabla ya Juni 2022 hasa ikizingatiwa hakuna tatizo la fedha ili Watanzania waanze kunufaika mapema.
MG 3-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza Waziri wa Nishati Dkt. Medrad Kalemani mara baada ya kuweka Jiwe la Msingi mradi wa Ujenzi wa Kuzalisha umeme Megawati 2115 katika eneo la mto Rufiji katikati ya Morogoro na Pwani.
  • Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt Medard Kalemani amesema tayari wakandarasi wanaojenga mradi huo wamelipwa asilimia 15 ya fedha zote za mradi huo ambayo ni sawa na shilingi Trilioni 1.007 na kwamba ujenzi utahusisha bwawa la maji lenye uwezo wa kukusanya mita za ujazo Bilioni 33.2, Jengo la mitambo ya kuzalisha umeme litakalokuwa na mitambo 9, kituo cha umeme na njia ya kusafirishia umeme yenye urefu wa kilometa 135 hadi kufika Chalinze.
  • Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson amesema Wabunge wanampongeza Mhe. Rais Magufuli kwa utekelezaji wa mradi huo na wanaamini kuwa umeme utakaozalishwa utawasaidia Watanzania na pia kufanikisha miradi mikubwa inayotekelezwa katika awamu hii ikiwemo ujenzi wa reli na ujenzi wa viwanda.
MG 4-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akifurahia pamoja na viongozi wengine mara baada ya tukio hilo la uwekaji wa Jiwe la Msingi.
  • Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amesema kuanza kwa ujenzi wa mradi huo ni mafanikio makubwa ya Mhe. Rais Magufuli ambaye amedhamiria kuhakikisha kila nyumba ya Mtanzania inapatiwa umeme.
  • Waziri wa Nishati wa Misri amewasilisha salamu za Rais wa Misri, Mhe. Abdel Fattah El- Sisi ambaye ameahidi kufuatilia ujenzi wa mradi huo unaofanywa na kampuni za Misri na pia ameahidi kuwa nchi hiyo itaendelea kushirikiana na Tanzania katika nyanja mbalimbali ikiwemo kutoa udhamini wa masomo ya nishati jadidifu kwa wanafunzi 50 ambao watasaidia juhudi za kuongeza uzalishaji wa umeme hapa nchini.
MG 5-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia eneo la bonde katika mto Rufiji mara baada ya kuweka jiwe la msingi la mradi huo wa umeme.
  • Aidha, Mhe. Rais Magufuli amewataka Watanzania kujivunia mafanikio haya makubwa ya kuongeza uzalishaji wa umeme nchini na kutoyumbishwa na wanaopinga utekelezaji wa mradi huo kwa kigezo cha uharibifu wa mazingira kwani mradi huo utasaidia zaidi kutunza mazingira kwa watu kutumia umeme badala ya kuni na mkaa zinazotokana na ukataji wa miti, na pia utasaidia kuwepo uvuvi, kilimo cha umwagiliaji na kuinua utalii kutokana na Wanyama wengi kupata maji ya uhakika.
  • “Kwenye hili pori la Selous kuna hoteli za kitalii za gharama kubwa, kuna vitalu vya utalii 47 na kuna uwindaji unaendelea, sasa haiwezekani sisi tukitaka kujenga bwawa la kuzalisha umeme tuambiwe tunaharibu mazingira wakati eneo tunalotumia ni chini ya asilimia 3 ya pori la Selous.
MG 6-01
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akikata utepe kuashiria uzinduzi wa mitambo itakayotumika katika mradi huo mkubwa wa kufua umeme.
  • Mradi huu umekumbana na upinzani mkali wa ndani na nje ya nchi, lakini kwa kuwa sisi ni Taifa huru na sio masikini kama watu wanavyodhani, tumeamua kutekeleza mradi huu” amesema Mhe. Rais Magufuli.
  • Mhe. Rais Magufuli ameagiza kumegwa kwa sehemu ya Pori la Akiba la Selous ili iwe Hifadhi ya Taifa na amependekeza iitwe Hifadhi ya Nyerere na sehemu yenye vitalu vya uwindaji iendelee, lengo likiwa kuimarisha zaidi uhifadhi wa maliasili katika eneo hilo na kupata manufaa zaidi.
MG 7-01
Eneo la mto Rufiji ambalo litatumika katika ujenzi huo wa kufua umeme kama linavyoonekana.
  • Ameagiza barabara ya kuunganisha eneo la mradi huo mpaka Fuga ianze kujengwa kwa kiwango cha lami hatua kwa hatua ili kurahisisha mawasiliano ya eneo hilo.Pamoja na kutaka wananchi wa Morogoro na Pwani wapewe kipaumbele katika ajira wakati wa mradi huo, Mhe. Rais Magufuli ameagiza mradi huo kukatiwa bima ya Taifa, utoaji wa vibali vya kazi kwa wafanyakazi wa kutoka nje ya nchi ufanyike haraka na vyombo vya ulinzi na usalama vya Morogoro na Pwani vishirikiane kuulinda.
  • Pia amewataka viongozi na wananchi wa Mikoa yote yenye vyanzo vya maji vinavyomwaga maji yake katika mto Rufiji kuhakikisha wanavitunza vyanzo hivyo ili viendelee kuchangia maji mengi katika mto Rufiji.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Ad

Rufiji

Ad

Unaweza kuangalia pia

RAIS MAGUFULI ATEMBELEA DAR ES SALAAM ZOO, AVUTIWA NA WANYAMA WENGI WANAOFUGWA HUMO

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *